Ulawiti, ubakaji na ndoa za utotoni ni mwiba wenye sumu Dar es Salaam

Ulawiti, ubakaji na ndoa za utotoni ni mwiba wenye sumu Dar es Salaam

Ingawa mapambano dhidi ya matukio mbalimbali ya manyanyaso ya kijinsia kwa watoto (wakike na kiume) yamekuwa yakifanyika katika jitihada za kupunguza ama kumaliza, lakini uchunguzi nilioufanya umebaini kwamba bado kuna haja ya kuongeza kasi ya mapambano hayo!
Binafsi nimekuwa nikipokea taarifa za matukio mbalimbali toka kwa wananchi na kuyarusha kupitia kipindi cha Hatua Tatu (katika kipengele cha Habari Ndio Hii).
 katika utafiti huo, nimebaini mambo mengi ambayo yanaweza kuzorotesha ama kupunguza jitihada zinazofanywa na taasisi mbalimbali za kiserikali na zisizo za kiserikali katika kupambana na matukio ya aina hiyo.
Uchunguzi umebaini kwamba, baadhi ya matukio ya ubakaji, ulawiti na ndoa za utotoni yanafanywa na watu wa karibu na watoto hao huku wakati wengine baba, kaka ama wajomba wakihusika moja kwa moja!
“Kila mmoja wetu huko mitaani ambako watoto wanakuwa wanacheza inabiti tuwajibike katika kuwa walinzi wazuri wa watoto wetu kwa sababu tafiti zetu zinaonyesha matukio ya ulawiti na ubakaji kwa kiwango kikubwa yanafanywa na watu wa karibu na watoto hawa wakiwemo akina baba, wajomba na hata kaka.” Aliwahi kunukuliwa Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Hellen Kijo-Bisimba.
Kijo-Bisimba ambaye kitaaluma ni mwanasheria, akiongea na Times Fm, alisema jamii inalazimika kutambua umuhimu wa watoto na kuwalea kimaadili sambamba na kuwapa elimu bora kwa faida yao na taifa kwa ujumla.
Aidha, taarifa ambazo Times Fm ilizipata mwaka jana kuhusiana na ukubwa wa matukio ya ulawiti na ubakaji kwa mkoa wa Ilala,  watoto zaidi ya 176 walibakwa na kunajisiwa, mkoa wa Temeke walikuwa watoto zaidi 209 huku mkoa wa Kinondoni wakilawitiwa na kubakwa watoto zaidi ya 197!
Hata hivyo, takwimu hizo ni zile ambazo kesi zake zilifikishwa Mahakamani achilia mbali zile ambazo ziliripotiwa katika vituo vya polisi na kushughulikiwa kindugu!
Kwa mujibu wa Makamanda wa polisi wa mikoa husika, Temeke, Ilala na Kinondoni, jitihada na elimu bado inaendelea kutolewa ndani ya jamii katika kuelewa umuhimu wa mtoto lakini pia wazazi na walezi kuachana na matukio hayo!
“Imani za kishirikina ni moja ya changamoto ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa sana matukio ya wazazi na walezi kufanya ngono na watoto wao, awali imani hizi zilikuwa nyingi zaidi mikoani lakini sasa changamoto hii imekuja hadi jijini Dar es Salaam hususani ndani ya mkoa wangu wa Ilala lakini kama jeshi la polisi tutambana na imani hizi katika kupunguza ama kumaliza tatizo hili.
“Kikubwa hapa tunachokiona baada ya uchunguzi wetu ni elimu tu ndani ya jamii kujitambua, lakini pia kupitia upya uhalali wa ufanyajikazi kwa hawa ndugu zetu wa tiba asilia (waganga wa kienyeji), baada ya kupitia vibali vyao nadhani tutajua tatizo lipo wapi na vipi tunaweza kupunguza ama kumaliza,” RPC wa Ilala,  Marietha Minangi alinukuliwa alipokuwa akizungumza na Times Fm.
Uchunguzi nilioufanya kwa hisani ya Times Fm na kuthibitishwa na Kamanda Minangi, Mkoa wa Ilala ni miongoni mwa mikoa iliyoathirika zaidi na matukio ya ubakaji sambamba na ndoa za utotoni.
“Pamoja na uwepo wa matukio hayo,  jeshi langu kwa kushirikiana na mmamlaka zinazohusika tumejitahidi kupambana nayo katika kuleta usawa miiongoni mwa jamii na ustawi wao kwa ujumla,” Minangi alisema.
Sehemu ambazo zinaonekana kuathirika zaidi na ndoa za utotoni ndani ya mkoa wa Ilala ni pamoja na Gongo la Mboto, Kivule, Chanika, Kinyerezi na Kitunda.
 Hakika, huu ni mwiba ndani ya jamii ya watanzania na unapaswa kutolewa kwa juhudi zote bila kujali uhusiano wa watenda makosa ya aina hii.
 - TimesFm

Post a Comment

أحدث أقدم