Phiri ashukuru 'kiama' kusogezwa

Kocha wa Simba Patrick Phiri
Kocha wa Simba Patrick Phiri amesema amefurahia mno kusogezwa mbele kwa mchezo wa watani wa jadi wa ligi kuu ya Bara dhidi ya Yanga kwa kuwa kikosi chake kinakabiliwa na rundo la majeruhi kwa sasa.
 
Akizungumza na gazeti hili jana kwa njia ya simu, Phiri alisema Simba ina majeruhi ambao wasingeweza kucheza dhidi ya Yanga katika tarehe ya awali Oktoba 12, kwenye Uwanja wa Taifa.
 
"Kwangu ni habari njema," alisema Phiri aliye katika awamu ya tatu ya uongozi wa benchi la ufundi la Simba alipoulizwa kama kuahirishwa huko kumeingilia programu yake yoyote. "(Kwa kusogezwa mbele) Sasa Ivo anaweza akawa amepona mpaka kufikia mchezo huo pamoja na Issa Rashidi na (Harun) Chanongo.
"Nimepata nafasi ya kuandaa timu ukizingatia mchezo dhidi ya Yanga ni mchezo mkubwa."
 
Pambano linaloibeba ratiba ya ligi kuu ya Bara la watani wa jadi hao limeahirishwa na shirikisho la soka (TFF) ili kupisha mchezo wa kimataifa wa kirafiki baina ya Taifa Stars na Benin siku hiyo.
 
Wachezaji wanne wa kikosi cha kwanza wa Simba wapo nje kwa sasa na walitegemewa kuukosa mchezo wa leo dhidi ya Polisi Morogoro na pambano hilo dhidi ya Yanga mabingwa wa mwaka jana.
 
Majeruhi hao ni mshambuliaji Paul Kiongera ambaye atakuwa nje ya uwanja kwa miezi miwili akiuguza goti, golikipa Ivo Mapunda ambaye ameumia kidole na atakuwa nje kwa wiki mbili. Wengine ni beki Issa Rashid na Harun Chanongo ambao wanauguza maumivu ya misuli.
 
Baada ya kusogezwa mbele huko Chanongo, Ivo na Rashid wanaweza kucheza dhidi ya Yanga kwa kuwa wanaendelea kupona.
 
Wakati huo huo, kocha wa Simba Patrick Phiri amesema timu yake imepania kushinda leo dhidi ya Polisi kwenye Uwanja wa Taifa baada ya kuachia uongozi wa mabao mawili na kutoka sare ya 2-2 dhidi ya Coastal Union Jumapili iliyopita.
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

أحدث أقدم