Adhabu ya kifo kwa kuritadi siyo haki katika Uislamu: mwanazuoni wa Somalia

Mahojiano na Bosire Boniface huko Garissa

Mwandishi wa Somalia Abdisaid Abdi Ismail amekuwa katika uchunguzi mkali baada ya kuchapisha kitabu kilichoandikwa kwa lugha ya Kisomali chenye jina "Sheria ya Uasi dini katika Uislamu: Je ni sahihi?" ambapo ametoa hoja kwamba hakuna uhalalishaji wa kidini wa mauaji ya watu kwa sababu ya kuasi dini.

Mkaazi wa Garissa akiwa na nakala ya kitabu "Xadka Riddada Maxaa Ka Run Ah?" ("Sheria ya Kuritadi katika Uslamu: Je ni Sahihi?") tarehe 24 Oktoba, 2014. [Bosire Boniface/Sabahi]

Kitabu hicho kimeibua majibu mchanganyiko miongoni mwa jamii ya Kisomali nchini Kenya na Somalia kufuatia uzinduzi wake huko Nairobi tarehe 14 Septemba.

Baada ya maulamaa kadhaa kutoa wito wa kitabu hicho kupigwa marufuku na kuchomwa, Maduka mengi ya kuuza vitabu ya Wasomali huko Eastleigh yameacha kuuza kitabu hicho, na sasa kinauzwa "kwa tahadhari" katika maduka machache ya kuuza vitabu huko Garissa na Nairobi na pia kupitia mtandao, Ismail alisema.

Ismail, raia wa Galkayo mwenye umri wa miaka 50 alipata udhamini wa masomo kutoka chuo kikuu cha Umm al-Qura huko Mecca, Saudi Arabia, ambapo alisoma sheria ya didni na uraghibishi, alihitimu 2002 shahada ya uzamili katika masuala ya uchumi wa Uislamu. Kutokea hapo, Ismail ameandika vitabu viwili kwa Kiarabu, "Nchi za Kiislamu' Kuongeza Mtaziko wa Madeni" na "Dunia kuwa kijiji kimoja katika Dunia ya Kislamu: Ukweli na Takwimu", na vitabu vingine viwili kwa Kisomali, "Saboolnimada sidee looga baxaa?" na "Hordhaca Dhaqaala Islaamka".

Mwandishi wa Somalia Abdisaid Abdi Ismail. [File]

Ismail, baba wa watoto watatu, anafundisha uchumi katika chuo kikuu cha Afrika Mashariki huko Bosaso tangu 2009, lakini amesema hawezi kurudi Somalia sasa kwa vitisho vya kifo ambavyo amekuwa akipokea kutoka alipochapisha kitabu hicho kipya huko Nairobi.


Katika mahojiano ya kina na Sabahi, Ismail alizungumza juu ya umuhimu wa kujadili mada ya uasi dini katika Uislamu, utafiti wake kuhusu mada hii, na umuhimu wa kuhamasisha na kuhimili mjadala wenye tija kuhusu mawazo tofauti miongoni mwa Wasomali.

Sabahi: Tuambie zaidi kuhusu kitabu chako na kwa nini ulikiandika.

Abdisaid Abdi Ismail: Mawazo makuu ya kitabu hiki ni kuhusu uasi dini katika Uislamu, lakini pia kinazungumza kuhusu masuala mengine kadhaa kama vile dola na dini, usawa wa kijinsia kulingana na fedha zinazolipwa fidia kwa familia ya mtu aliyeuawa, kifo kwa kuwapiga mawe wanaume na wanawake wazinifu, na kadhalika.

Niliandika kitabu hiki kwa jamii ya Wasomali kuwafanya wajue baadhi ya masuala muhimu katika dini yao ambayo yanahusisha maisha yao katika dunia hii na baada ya hapo, ambayo baadhi ya Maulamaa wa Kisomali wamekuwa wakieleza mara kwa mara kwa namna ambayo haiendani na maana halisi ya mafundisho ya Kiislamu.

Ni matumaini yangu kwamba anayesoma kitabu hiki atagundua kinachosemwa na Uislamu kuhusu masuala yaliyozungumziwa katika kitabu hiki, lakini ujumbe muhimu ni kwamba Uislamu ni dini inayojali ubinadamu na msamaha, na maadili yake yanahusu maisha ya binadamu.

Sabahi: Umefanya suala la kuritadi kuwa lengo kuu. Kwa nini unafikiri ni muhimu sana kwa sasa na muhimu kwa Wasomali kuelewa?

Ismail: Ni suala muhimu sana katika jamii ya [Uislamu] leo hii kwa sababu vikundi vya wenye msimamo mkali vinatumia suala la uasi wa dini kama nyenzo ya kuhalalisha mauaji yao ya kutisha na ya kikatili dhidi ya wale wanaopinga tafsiri yao yenye makosa ya Uislamu au hata ajenda yao ya kisiasa.

Suala hili ni muhimu sana kwa jamii ya Kiislamu kwa ujumla, lakini hasa kwa jamii ya Somalia, kwa sababu damu yao inamwagwa kila siku kwa kutumia uasi wa dini kama nyenzo ya kulihalalisha.

Nafikiri mada inastahili kujadiliwa katika namna pana katika hali ya sasa ya ulimwengu wa Kiislamu. Ningependa kama mtu mwingine angeweza kuandika kuhusu hilo, lakini bahati mbaya hakuna aliyeandika kuhusu hilo na hilo limenilazimisha kufanya hivyo sasa, na ninachagua lugha ya Kisomali ili niweze kuwafikia watu wanaozungumza Kisomali Afrika Mashariki na duniani kote kwa ujumla.

Sabahi: Je, kifo ni adhabu inayofaa kwa kuritadi na kulingana na mafundisho ya Kiislamu?

Ismail: Nimekuwa nikifanyia utafiti suala la kuritadi kwa kipindi kirefu sasa, nikilinganisha mitazamo mbalimbali na ushahidi ambao kila kikundi cha msimamo mkali kinautumia na Korani na mafundisho ya mtume yanasemaje kuhusu hilo.

Kilichofanya ugunduzi wangu kuhitimishwa ni kwamba adhabu ya kifo kwa uasi wa dini haina hoja yoyote ya halali katika Uislamu ingawaje imekuwa ikitumika kwa karne nyingi kwa madhumuni ya kisiasa kwa wasomi wanaotawala katika msururu wa utawala wa kihistoria wa Uislamu kama njia ya uhaini kwa Waislamu ambao wanaacha dini, kwa sababu dini ilikuwa utambulisho wa pamoja kwa watu wakati huo.

Sabahi: Je, utafiti wako unasema adhabu sahihi ni ipi kwa uasi wa dini kwa mujibu wa Uislamu?

Ismail: Kwa kuzingatia uhakiki wa wanazuoni wa mafundisho ya dini, maoni yangu kuhusiana na uasi wa dini ni kwamba hakuna adhabu ya uasi wa dini katika ulimwengu huu. Adhabu iko katika maisha ya mbinguni na ni kati ya mtu na Mungu.

Uhuru wa dini na imani ni baadhi ya haki za msingi za binadamu na hakuna mtu mwenye haki ya kuingilia kile ambacho wengine wanaamini. Mawazo na maoni tofauti na mbalimbali ni muhimu sana kwa kuishi pamoja, kuelewana na maendeleo ya jamii yoyote.

Sabahi: Kwa nini Waislamu wanapaswa kusoma kitabu hiki?

Ismail: Wanapaswa kukisoma kwa sababu wanahitaji kujua ukosefu wa uhalali halisi kwa adhabu ya uasi wa dini katika Uislamu, ambao nimeridhika kwamba hakuna uungaji mkono halali kuruhusu adhabu ya kifo kwa uasi wa dini katika Uislamu.

Kitabu kitafafanua kwa wasomaji masuala mengine mengi moja kwa moja au isivyo dhahiri kuhusiana na suala la uasi wa dini na inategemewa kitashawishi vikundi kuacha kutumia [suala hili] kuua watu [kwa kuzingatia] uhalalishaji wa kupotosha.

Ninatumaini kwamba wakati [idadi ya] watu wanaosoma kitabu inaongezeka, uendawazimu unayoikumba nchi yetu utapungua kidogo na hatimaye vijana watatambua kuwa wanatumiwa dhidi ya watu wao chini ya kisingizio cha kutokuwa Waislamu.

Sabahi: Kitu gani kinakosekana katika mazungumzo miongoni mwa Wasomali wanapojadili masuala na mawazo haya?

Ismail: Vipengele kadhaa vinakosekana katikajambo hili, kama vile kufikiria kwa kina na wanazuoni wapya ambao wanaweza kutafsiri Kuran na hadithi (mafundisho ya Mtume Mohammed) kwa mujibu wa muktadha wake wa asili bila ya upendeleo wa vikundi mahususi ambavyo vinataka kuuteka Uislamu kwa manufaa yao wenyewe.

Kunatakiwa kuwa na mazungumzo ya wazi na huru miongoni mwa wanazuoni na ujumbe wa namna ya kutafsiri vyanzo vya Kiislamu katika njia ambayo inaweza kusaidia Waislamu kuishi kistaarabu na kwa uvumilivu kama wanavyopaswa kuishi, ili iwawezeshe kuishi kwa amani miongoni mwao wenyewe na wengine katika dunia yetuu hii.

Sabahi: Je, nini ni chanzo cha itikadi ya al-Shabaab?

Ismail: Ninaamini kwamba al-Shabaab na vikundi vingine vinavyofanana na hicho wanatekeleza tu mafundisho na uelewa wa baadhi ya wanazuoni wa kiislamu ambao wanatafsiri baadhi ya vifungu vya kiislamu kwa mujibu wa ajenda zao.

Kupata uelewa wa al-Shabaab na wenye msimamo mkali wengine, kwanza tunapaswa kufafania Kuran na masimulizi na vyanzo vingine vya Kiislamu kutokana na maandiko yake halisia. Vita dhidi ya al-Shabaab na wengine wenye msimamo mkali ni vita vya mioyo na akili za jamii ya Kiislamu na kuvishinda vita hivyo tunapaswa kurejea hali halisi ya Uislamu ambayo ni ya amani, uvumilivu na ya kidemokrasia.

Sabahi: Vikundi kama vile al-Shabaab wanadai kujaribu kuunda jamii halisi kama ilivyokuwa wakati wa Mtume Mohammed. Je, ni kipi kibaya kwa kufanya hivyo?

Ismail: Hakuna lililo baya, lakini ni nani anayewasilisha hilo? Hoja langu ni kwamba tunatakiwa kuelewa Uislamu halisi, na sio Uislamu wa kisiasa.

Kwa upande mwingine, tunapaswa kuzingatia tofauti kati ya kipindi ambacho Mtume Mohammed, amani iwe juu yake, na alioishi nao wakati huo, na dunia yetu, katika karne ya 21, wakati hali ya maisha ni tofauti kabisa.

Sabahi: Je,ulitarajia majibu hasi kwa kitabu chako?

Ismail: Kwa kweli, nilitarajia kitabu hiki kuanzisha mjadala wa kitaaluma miongoni mwa wanazuoni, lakini kamwe sikutarajia kwamba mtu fulani atatoa wito wa kukizuia kitabu hicho na kutangaza kuwa mwandisi ni muasi wa dini.

Hilo ndilo jambo ambalo kitabu hiki kinajaribu kuzungumzia na inaonekana wale waliopo katika msimamo mkali hawakuelewa kabisa ujumbe mkuu wa kitabu hicho, ambao ni [kuhamasisha] mazungumzo na mjadala.

Hata hivyo, kumekuwa na majibu chanya kutoka kwa watu mbalimbali ambao wanasema muda ulikuwa sahihi kuibua suala hilo.

Sabahi: Je, unafanyaje na nini kitakachofuata kwako?

Ismail: Nilikuja Nairobi kutoka Somalia mwezi Agosti mwaka huu kwa lengo la kuchapisha kitabu hiki kwa kuwa hakuna wachapishaji nchini Somalia. Kama kungekuwa na wachapishaji nchini Somalia, hata hivyo wasingekuwa tayari kuchapisha kitabu hiki.

Sasa ninajaribu kujiokoa kutoka kwa baadhi ya watu wenye itikadi kali na wafuasi wao ambao hawajazificha nia zao za kunidhuru badala ya kitabu changu. Mienendo yangu ni ya siri na imepunguzwa, mara nyingi ninakuwa ndani ya nyumba.

Wakati huo huo, ninaaandika kitabu kingine kinachousu namna Uislamu wa amani unavyoweza kusambazwa miongoni mwa jamii ya Somalia. Sitazuiliwa wala kutishwa kutokana na mazungumzo na kujadili masuala ambayo ninaona ni muhimu kuleta Uislamu halisi na sahihi kwa jamii nyingi. Nitaendelea kurejelea ukweli kuhusu msimamo sahihi wa dini kuhusu masuala kadhaa ambayo nimeyazungumzia katika kitabu hiki na [masuala] mengine.

Post a Comment

Previous Post Next Post