Utata wa Miss Tanzania, Sitti Mtemvu kulivua Taji hilo

Siku moja baada ya Miss Tanzania 2014, Sitti Mtemvu ‘kueleza’ kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii Facebook kulivua taji hilo, waandaaji wa mashindano hayo, Lino Agency International wamesema hawajapokea barua rasmi kutoka kwa mrembo huyo ya kulivua taji hilo. 
 
Juzi zilizagaa taarifa kuwa mrembo huyo amelivua taji baada ya kuwapo ujumbe katika mtandao wa facebook ambao unaonyesha umeandikwa na mrembo huyo. Ujumbe huo ulisomeka:
 
“Habari za jioni Watanzania wenzangu, kutokana na kusemwa maneno mengi yasiyo na tija juu ya hili taji la Umiss Tanzania mpaka kusababisha nisiwe na amani na uhuru ndani ya nchi yangu, kwa roho safi nimeamua mwenyewe kulivua taji hilo na kuacha wanayeona anastahili apewe ili niendelee na maisha yangu kwa amani, isiwe shida sana kwani sitegemei taji hili ili kuishi.”
 
Hata hivyo, taarifa ambazo tumezipata zinasema, Sitti alifikia uamuzi wa kulivua taji baada ya kushauriwa kufanya hivyo na wizara inayosimamia habari, vijana, utamaduni na michezo ambayo ilifanya kikao juzi na Mkurugenzi wa mashindano hayo, Hashimu Lundenga na Katibu Mkuu wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Godfrey Lebejo.
 
Inaelezwa kuwa kikao hicho kilifanyika kwa ajili ya kutafuta ukweli kuhusu suala la umri wa Sitti, kwani nyaraka mbalimbali za mrembo huyo zinaonyesha amezaliwa Mei, 1989 hivyo ana umri wa miaka 25 wakati moja ya vigezo ambavyo mshiriki wa mashindano ya Miss Tanzania anatakiwa kuwa navyo ni kuwa na umri usiozidi miaka 24.
 
Wiki iliyopita Sitti aliingia kwenye kashfa zaidi ya kudanganya umri baada ya kuibuka na cheti kipya cha kuzaliwa ambacho kinaonyesha alizaliwa Mei 31, 1991 wakati zipo nyaraka zinaonyesha alizaliwa mwaka 1989. Nyaraka hizo ni hati yake ya kusafiria na leseni ya udereva ambayo ilitolewa nchini Marekani.
 
Chanzo chetu cha habari kinasema, katika kikao kilichoandaliwa na Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo yalifanyika majadiliano ya kina ikiwa ni pamoja na kulinda heshima ya baba yake Sitti ambaye ni Mbunge wa Temeke, Abbas Mtemvu kwa hiyo mrembo huyo alishauriwa atangaze mwenyewe kuvua taji hilo.
 
“Kikao cha Kamati ya Miss Tanzania na familia ya Mtemvu kitakaa jioni (jana), Sitti mwenyewe ndiye atatakiwa kutangaza kujivua taji hilo, nadhani baadaye  utatolewa msimamo wa familia ila mpango uliopo ni Sitti aachie taji hilo,” kilisema chanzo hicho cha habari.

Post a Comment

أحدث أقدم