Anne Kilango aichapa serikali

MBUNGE wa Same Mashariki, Anne Kilango (CCM), ameilipua Serikali kuwa kutokana na kuwa legelege ndio maana nchi za nje zimeifanya Tanzania kuwa sehemu ya kuuzia  dawa za kulevya.
Kilango alitoa kauli hiyo jana bungeni wakati akiuliza swali la nyongeza kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Uratibu wa Bunge, William Lukuvi.
Alisema kuwa baadhi ya nchi za nje yakiwemo mataifa ya Nigeria na Pakistan, yameiona Tanzania ndio nchi ya kuuzia dawa hizo za kulenya kutokana na kuwa legelege, jambo ambalo ni hatari.
Pia, Mbunge huyo aliihoji Serikali kwanini isiendeshe kesi zinazohusiana na dawa za kulevya kwa siku 14 ili kuondoa mianya ya rushwa.
Aidha, Kilango aliitaka Serikali iweke wazi suala la uteketezaji wa dawa hizo za kulevya kwa wananchi ili nao waweze kujiridhisha kuhusiana na uteketezwaji huo.
Akijibu swali hilo, Lukuvi alisema kuwa sheria ya kupambana na dawa za kulevya ina mapungufu makubwa sana hata ikilinganishwa na nchi ya Bangladesh, kwani Wakili wa nchi hiyo hukaa uwanja wa ndege na mtu anapobainika kukutwa na dawa hizo, husomewa kesi yake hapo hapo.
“Sheria yetu ina mapungufu makubwa na kutokana na mapungufu haya, hivi sasa tupo katika utaratibu wa kuleta Muswada wa Sheria ya kupambana na dawa za kulevya ili kuweza kukabiliana na tatizo hili, kwani hapa nchini hata mtu ukimkamata na dawa hadi zipelekwe kwa Mkemia Mkuu wa Serikali,” alisema.
Katika swali la msingi, Mbunge huyo alitaka kujua mara dawa za kulevya zinapokamatwa huwa zinapelekwa wapi?
Akijibu swali hilo, Lukuvi alisema kuwa dawa za kulevya zilizokamatwa huhifadhiwa na kutumika mahakamani kama vielelezo katika uendeshaji wa kesi husika.
“Baada ya kesi kukamilika, dawa hizo huharibiwa au kuteketezwa kwa amri ya mahakama kama ilivyoelekezwa katika kifungu cha 34 cha Sheria ya kupambana na biashara haramu ya dawa za kulevya sura ya 95,” alisema.
Lukuvi, alisema uteketezaji wa dawa hizo za kulevya umewahi kufanyika mwaka 2012, ambako kilo 92.2 za Heroin zilitekelezwa katika Kiwanda cha Saruji Tanga kwa amri ya mahakama, ambako mwaka 2013 kilo 412.7 za bangi ziliteketezwa, kilo 12.3 za Heroin na kilo 5.6 za Cocaine ziliteketezwa katika kiwanda cha Saruji Wazo Hill jijini Dar es Salaam

Post a Comment

أحدث أقدم