Tandahimba. Baada ya kupata mafanikio ya
wastani katika kilimo cha ufuta, wakulima wa zao hilo, ambao wengi ni
wale wanaohama makazi yao kwa muda kutoka Wilaya ya Tandahimba, Mtwara
kwenda Lindi kwa ajili ya zao hilo, sasa wanalilia elimu ili waweze
kupata mafanikio makubwa zaidi.
Baadhi yao wanasema licha ya kwamba wanafanya kazi
hiyo kwa bidii kutokana na faida na matokeo mazuri ya haraka
wanayoyapata, hakuna mtaalamu yeyote wa kilimo ambaye aliwahi
kuwaelekeza kuhusu namna bora ya kilimo hicho.
Kati ya Novemba na Mei mamia ya wakulima katika
Wilaya ya Tandahimba huyaacha makazi yao na kwenda kuishi mkoani Lindi
katika wilaya za Liwale na Kilwa kwa ajili ya kusaka ardhi yenye rutuba
inayofaa kwa kilimo cha ufuta.
Mbali na ardhi yenye rutuba, wananchi wa
Tandahimba wanasema eneo kubwa linalofaa kwa kilimo katika wilaya yao
limefunikwa na zao la kudumu la mikorosho, hivyo ardhi iliyobaki
haitoshelezi kumudu mahitaji ya kilimo cha mazao mengine, ufuta likiwa
mojawapo.
“Hakuna mtaalamu yeyote wa kilimo aliyetueleza
kilimo bora cha ufuta, tunachotumia ni uzoefu kwa kuwa tunafahamu ufuta
ni zao linalohitaji rutuba nyingi basi tunakimbilia maeneo yenye rutuba
hiyo,” anasema Mohamed Kawanga ambaye ni mkulima wa Kijiji cha Mkwiti,
Tandahimba na kuongeza:
“Ukilima hapa Tandahimba utalazimika kutumia
mbolea nyingi kwa zao la ufuta ambayo ni gharama kubwa, wakati mtu
ukienda Lindi kuna eneo kubwa lenye ardhi nzuri, hivyo ni rahisi kulima
na hakuna gharama za ziada.”
Wilaya ya Tandahimba ina wakazi 227,514 kwa mujibu
wa sensa ya watu na makazi ya 2012, wanaoishi katika kilomita za mraba
2048.56, ambazo kati yake asilimia 90 zinafaa kwa kilimo.
Hata hivyo, asilimia 91 ya eneo linalofaa kwa
kilimo limefunikwa na miti ya mikorosho ambayo ndiyo uti wa mgongo wa
uchumi wa wakazi wake. Wilaya hiyo inaoonga za uzalishaji wa korosho
ambapo msimu 2013/14 ilizalisha tani 32,000.
Siyo lazima kuhama
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa kama
wakulima wa Tandahimba wangekuwa na elimu kuhusu kilimo cha zao hilo,
pengine wasingelazimika kusafiri hadi nje ya mkoa wao kwa ajili ya
kilimo cha ufuta, kwani elimu hiyo ingewawezesha kulima zao hilo katika
wilaya yao, hoja ambayo inaungwa mkono na wataalamu wa kilimo mkoani
Mtwara.
Mkazi wa Nannala, Rashidi Mkadimba anasema kilimo
cha ufuta kinaendeshwa kwa mazoea kutokana na wakulima kutokuwa na elimu
ya kilimo hicho.
“Sisi kwetu hapa Nannala hatujui chochote cha
kitaalamu kuhusu kilimo cha ufuta, hata huko Lindi tunapokwenda tunalima
tu bila kufuata kanuni za kilimo kutokana na kutozifahamu,” anasema
Mkadimba.

إرسال تعليق