Fomu Serikali za mitaa utata

Katibu Mkuu wa TAMISEMIWAKATI fomu za kugombea ujumbe wa Serikali za Mitaa zikianza kutolewa rasmi jana, zimelalamikiwa na vyama vya siasa kwamba maelezo yake yanatatanisha hususani kifungu cha 21 na 22, ambako mgombea anatakiwa kujaza nembo ya chama chake na halmashauri.
Suala hilo, liliwahi kulalamikiwa na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, wakati akisoma maazimio ya Kamati Kuu ya chama hicho iliyoketi hivi karibuni, akisema kuwa wamebaini kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinataka kutumia mbinu hiyo kuwaengua wagombea wa upinzani watakaoshindwa kutimiza matakwa ya vifungu hivyo.
Kwa mujibu wa fomu hiyo ambayo Tanzania Daima limeona nakala yake, mgombea anatakiwa kujaza nembo ya chama chake na halmashauri bila kufafanua anatakiwa kuzitaja alama zilizopo kwenye nembo hizo ama kuzichora, suala ambalo limeibua utata mkubwa kwa wagombea.
Mkurugenzi wa Bunge na Halmashauri wa CHADEMA, John Mrema, alizungumzia utata huo kuwa ni mbinu chafu iliyoandaliwa kwa makusudi ili kuvuruga uchaguzi huo, jambo alilosema hawako tayari kwa hilo.
“Jambo hili tulimwandikia barua rasmi Waziri Mkuu na mpaka leo mwezi mmoja umeishia hakuwahi kulitolea ufafanuzi wowote, achilia mbali kujibu barua yetu tuliyomuandikia kutaka ufafanuzi huo na hata alipotoa mwongozo wa uchaguzi huu, hakulizungumzia hata kidogo.
“Ukisoma fomu zilizoanza kutolewa leo SEHEMU A: Maelezo ya Mgombea, utaona kuwa kifungu cha 21 na 22 ndivyo vinamtaka mgombea kujaza nembo ya chama chake na ya halmashauri yake,” alisema.
Mrema, alifafanua kuwa jambo hilo limewachanganya sana wanachama wao hasa kitendo cha kumtaka mgombea ajaze nembo ya halmashauri na ya chama chake, kwamba ikumbukwe kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), amenunuliwa na magazeti akisema kuwa wanasiasa wanaozungumzia suala la nembo ni porojo na hakuna kitu kama hicho.
“Kabla hata ya wino ulioandika maneno yake haujakauka ametoa fomu ambazo zinataka mgombea kujaza nembo ya chama na ya halmashauri, hizi ni dalili za wazi kuwa serikali hii imefikia ukomo wa kufikiri na haipo makini hata kidogo, inayumba na imepoteza mwelekeo,” alisema Mrema.
Alisisitiza kuwa, wanataka Tamisemi watoe ufafanuzi wa kina kuhusu fomu hizo kama ni halali kwa mgombea kutakiwa kujaza nembo ya halmashauri na ya chama chake, kwamba ijulikane wazi kuwa kuchora nembo hizi ni kazi ngumu sana, kwani nyingine ni vigumu kuzichora.
“Tunataka waeleze kama ni halali kwa mgombea atakayeshindwa kujaza fomu hizi itakuwa kigezo kimojawapo cha kuwekewa pingamizi na hatimaye kuenguliwa kwenye uchaguzi husika, kwani ikiachwa kama ilivyo inasababisha vurugu katika uchaguzi huu,” alisema Mrema.
- Tanzania Daima

Post a Comment

أحدث أقدم