Kifanyike nini mihimili ya dola inapokinzana?

Tumeshuhudia kwa mara ya kwanza tangu nchi yetu ipate uhuru mwaka 1961, mihimili ya dola, yaani Mahakama, Bunge na Serikali ikigongana na kukinzana katika suala muhimu la kitaifa, huku ikiibua mashaka kuhusu tafsiri ya dhana ya mgawanyo wa madaraka miongoni mwa mihimili hiyo. Hali hiyo imetokana na amri ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam iliyodaiwa kuzuia Bunge kujadili ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuhusu kashfa ya uchotwaji wa Sh306 bilioni kwenye akaunti ya Tegeta Escrow.
Wakati mahakama hiyo ikidaiwa kutoa amri hiyo ambayo ingedumu hadi kesi ya msingi iliyofunguliwa katika mahakama hiyo na kampuni ya kufua umeme ya IPTL na kampuni tanzu ya Pan African Power Solutions (PAP) itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi, Bunge lilisema ripoti hiyo lazima ijadiliwe kwa kuwa linayo mamlaka kikatiba kuendesha shughuli zake bila kuingiliwa na mamlaka nyingine yoyote, ikiwamo Mahakama. Bunge lilisimamia kwenye ibara ya 100 (1) katika Katiba inayosema kuwa, kutakuwa na uhuru wa mawazo, majadiliano na utaratibu katika Bunge na uhuru huo hautavunjwa wala kuhojiwa na chombo chochote katika Jamhuri ya Muungano au katika Mahakama au mahali pengine nje ya Bunge.
Lakini ukweli uliojitokeza baadaye ni kwamba Mahakama Kuu haikuzuia Bunge kujadili ripoti hiyo ya CAG kuhusu kashfa ya akaunti ya Escrow. Ukweli ni kwamba mkanganyiko uliojitokeza ulitokana na Bunge kutoa matamko kuhusu kuwapo amri ya mahakama iliyodaiwa kuzuia mjadala wa ripoti ya CAG bila kuwa na nakala halisi ya hukumu husika. Hivyo, matamko ya wabunge yalikuwa hisia tu zisizokuwa na ukweli wowote. Ndiyo maana awali tulihoji kama kweli kuna mahakama yoyote nchini inayoweza kutoa amri inayokwenda kinyume na ibara hiyo ya 100 (1)ya Katiba inayotoa kinga kwa Bunge ili lisiingiliwe kwa njia yoyote katika kuendesha shughuli zake.
Ni kwa mantiki hiyo tunasema huenda amri ya Mahakama Kuu ilitafsiriwa vibaya kutokana na kujadiliwa bungeni na bila kwanza kuona nakala halisi ya hukumu ya mahakama hiyo. Inawezekana kabisa kwamba huenda hali hiyo ilisababishwa na mihemko ya kisiasa iliyotokana na unyeti wa kashfa hiyo ya akaunti ya Escrow. Ukweli ni kuwa, pamoja na juhudi za IPTL na PAP kuomba mahakama kuzuia mjadala huo bungeni, hukumu iliyotolewa na majaji hao ilisema kila kitu kiendelee kama kilivyopangwa, hivyo hakuna mahali popote katika amri hiyo, ambapo Bunge lilikatazwa kuijadili ripoti hiyo ya CAG.
Ingekuwa kweli kwamba mahakama ililizuia Bunge kujadili ripoti ya CAG, hapana shaka kwamba Mahakama ingekuwa imevunja Katiba kwa kuliingilia Bunge lisifanye shughuli zake. Pia lawama zingeelekezwa kwa mhimili huyo kwa kusababisha mkanganyiko huo, kama ambavyo zimekuwapo lawama kwa baadhi ya majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani kuandika hukumu kisiasa, kwa maana ya kuzungukazunguka na kutoa hukumu ambazo siyo tu hazieleweki, bali pia zenye maudhui yanayochanganya.
Ni katika muktadha huo tunasema kuna umuhimu wa kuanzisha Mahakama ya Katiba hapa nchini, ambayo jukumu lake litakuwa kushughulikia kesi na mashauri ya kikatiba iwapo yatatokea. Ripoti kuhusu kashfa ya Escrow iliyowasilishwa bungeni jana ni somo tosha kwa kila mmoja wetu na mihimili yote ya dola.

Post a Comment

Previous Post Next Post