
Juzi taasisi iitwayo Environmental Investigation
Agency (Wakala wa Uchunguzi wa Mazingira– EIA) ilitoa hadharani ripoti
ambayo inataja maofisa na wanausalama wa China kwamba walitumia fursa ya
kidiplomasia kusafirisha meno ya tembo kwa ndege ya Rais Jinping ambaye
alitembelea Tanzania Machi 2013.
Ikulu ya Dar es Salaam na Ofisi ya Mambo ya Nje ya
China kwa nyakati tofauti zilisema taarifa hizi siyo za kweli na jana
Serikali ya Tanzania kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa, ilitoa taarifa bungeni na kuziita taarifa hizo kuwa ni za
“kupikwa”.
Wakati hayo yakiendelea, ripoti hiyo ya EIA
iliyopewa jina la Vanishing Point: Criminality, Corruption and
Devastation of Tanzania’s Elephants (Hatua ya kutoweka: Uhalifu, Rushwa
na Kuangamizwa kwa tembo wa Tanzania), inafichua madudu zaidi yanayoweka
bayana jinsi uhalifu wa utoroshaji wa meno ya tembo unavyofanyika.
Ripoti hiyo inalitaja pori la akiba la Selous kuwa
kituo cha mauaji ya tembo, kwani matukio ya ujangili hupangwa katika
vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo, kisha kutekelezwa kwa msaada wa
polisi na baadhi ya wananchi.
Inavitaja vijiji vilivyopo katika maeneo ya Mloka,
Tunduru, Namtumbo, Liwale na Kilwa ambako wafanyabiashara wadogo kutoka
Dar es Salaam hukodishwa silaha na wawindaji, kisha kuingia katika
hifadhi hiyo na kufanya uhalifu.
“Wakati mwingine wawindaji kutoka nje ya eneo hilo
hutumiwa na baadhi ya maofisa kutoka serikalini,” inasomeka sehemu ya
ripoti hiyo.
Katika tukio la aina yake, ripoti hiyo imeeleza
tukio la katikati ya mwaka huu ambapo kundi la wawindaji kutoka Arusha
lilitumwa na maofisa wa polisi waliokuwa Mloka na kuingia katika hifadhi
hiyo kwa ajili ya kuwinda.
Inadaiwa kuwa maofisa hao wa polisi walitoa silaha
kwa kundi hilo la wawindaji na baada tu ya mauaji ya tembo wapatao
watano walichukua meno kutoka kwa wawindaji.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, tembo akishauawa, meno
yake hukatwa kisha kufukiwa hadi pale mnunuzi anapowasili ambapo
hufukuliwa na kupewa.
EIA katika ripoti hiyo inabainisha kuwa meno mengi
ya tembo kutoka Selous husafirishwa kwenda Dar es Salaam, ama kwa
kutumia barabara kwa maana ya magari ambayo yametengezwa maalumu kwa
ajili ya kazi hiyo, au kwa kupitia majini wakitumia mitumbwi ya asili.
“Wakati mwingine pikipiki hutumika kupitia njia za
vichakani kukusanya meno hayo kule ambako zimefichwa hadi kufikia
barabara kuu,” inasema sehemu ya ripoti hiyo. Kutoka kwenye njia kuu
husafirishwa kwa magari binafsi ambayo yanakuwa sehemu maalumu kwa ajili
ya kuficha pembe hizo au kupitia mabasi ambayo husafirisha meno ya
tembo zaidi kuliko abiria kutokana na malipo makubwa ambayo hutolewa kwa
kazi hiyo.
- Mwananchi
- Mwananchi
Post a Comment