Matibabu ya wakubwa yakiisha, tuulizie afya za hohehahe- 2

 
Jumapili iliyopita, tulijadili sehemu ya kwanza ya makala haya. Tuliangalia kwa muhtasari suala la Rais wetu kwenda kutibiwa nje ya nchi na kutoa taarifa kuwa utaratibu huo ni wa kawaida kwa marais na viongozi wengine hapa Afrika.
Tulitoa pole kwake, familia yake na Watanzania wote na kujenga hoja iliyohoji umuhimu na utaratibu wa viongozi wengi wa Afrika kuendelea kupata huduma bora za matibabu Ulaya na Marekani, huku nchi zao huduma zake za afya zinatia hofu. Tuliangalia takwimu za kimataifa juu ya masuala ya afya na kugusia Tanzania imesimamia wapi.
Tulionyesha kuwa Tanzania ikiamua kuboresha huduma zake za afya ili kila mmoja, mwenye cheo na asiye nacho, aliye mbunge na asiye mbunge na kadhalika, aweze kutibiwa hapa ndani ya nchi. Hilo linawezekana. Tulitoa mfano wa fedha za umma zilizoibiwa katika akaunti ya ESCROW Sh200 bilioni(wakati huo), sasa zikiwa Sh321 bilioni, baada ya taarifa ya CAG kuonyesha hivyo na kusisitiza kuwa fedha hizo zingeweza kabisa kututengenezea maelfu ya madaktari bingwa achilia mbali kama tungeamua kuziwekeza katika maeneo mengine ili kuboresha sekta ya afya.
Leo tutaendelea kuangalia udhaifu mkubwa na wa kimakusudi unaofanywa na Serikali yetu kwa jumla katika uboreshaji wa sekta ya afya na kutoa suluhisho la kudumu.
Kikombe cha Babu Loliondo
Alipotokea mzee wa Loliondo, tulishuhudia viongozi wakubwa wa Serikali wakikimbilia huko kwenda kunywa kikombe ili waponywe magonjwa yao. Viongozi hao walifanya hata wananchi wa kawaida waamini kuwa kikombe cha babu kinaponya, madege na misafari ya magari kutoka kila kona ya nchi vikaelekezwa Loliondo. Loliondo ikawa Loliondo. Watu wakawaondoa wagonjwa wao hospitalini ili wawapeleke Loliondo. Loliondo ilikuwa ni Kigezo cha ujinga na upuuzi wetu, kilionyesha ni namna gani tunaamini katika “tunguli na maajabu” kuliko kuwekeza katika matibabu salama, yanayoaminika, yaliyofanyiwa utafiti na yanayoisaidia dunia nzima. Matibabu ya hospitalini. Wengi wa waliodanganywa na Loliondo, hasa wagonjwa wa Ukimwi, walishafariki dunia. Loliondo ilikuwa ujanja mwingine na labda mradi wa wakubwa. Tunapenda sana mambo ya mchezo kama Loliondo, huku tukikataa kuboresha sekta yetu ya Afya.
Viongozi hawaamini hospitali zetu, madaktari wetu na vifaa vyetu
Hii ni kasumba mbaya kuliko zote Afrika. Viongozi wetu wengi hawaamini katika huduma zinazotolewa hapa nchini. Mara kadhaa wamesafiri kwenda nchi za nje na kuona miundombinu ya sekta ya afya ya nchi za wenzetu, wakiifananisha na hapa kwetu wanaona huku kwetu ni “upuuzi” mtupu na hakuwezekaniki. Kwa sababu kiongozi ndiye njia, njia inapoona mbele ni giza, maana yake mfuasi (mwananchi) hana cha kubadilisha.
Tuna viongozi lukuki katika Serikali yetu hawaamini kabisa kuwa sisi tuna hazina ya kutosha ya vijana ambao tukiwaendeleza na kuwapa taaluma za kigeni na kisha tukawanunulia vifaa, tukawapa mishahara mizuri, wakaishi katika nyumba nzuri na mazingira rafiki kidogo tu, wanaweza kufanya hayo tunayoyafuata Marekani na Ulaya kirahisi mno.
Ukishakuwa na Serikali ambayo haiwaamini askari wake, silaha zao na hata ujasiri wao katika kuipigania nchi yao, je utakuwa na jeshi linalofanya kazi kwa kujituma na kujiamini? Haiwezekani. Vita ikitokea wakubwa wanaenda kukodi majeshi ya wazungu na wakubwa wenzao waliondelea huko na kule ili kuwapigania, wakishaokolewa wanasifia majeshi ya nchi hayo kwa kuwasaidia vita ambayo kama tungejipanga, majeshi yetu yangepigana vita hiyo bila kukodi majeshi ya nje.
Ndiyo maana sekta ya afya inazidi kudorora kila uchwao, huku tukiwa tunaangalia. Ukienda vijijini, ndiko unaweza kulia, kuna vijizahanati ambavyo havina msaada. Wauguzi wamekata tamaa na kuna eneo lingine imeripotiwa hivi karibuni kwamba mlinzi alikuwa akihudumia waja wazito kwa sababu hakuna nesi wa kufanya hivyo. Utakuta mtu anakimbia hicho kijizahanati walau kwenda hospitali ya mkoa au wilaya, huko nako kunakatisha tamaa.
Kituko cha “Uric Acid’
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post