Mwamaja: Naishi na maumivu makali kwa miaka 34

Kocha wa Prisons, David Mwamaja ana mwonekano tofauti na makocha wengine wa Ligi Kuu Bara kutokana na mwili mkubwa alionao.
Hata hivyo, Mwamaja anasema ana maumivu ya goti ambayo yanamnyima furaha na amekuwa akiishi na maumivu hayo kwa miaka 34.
“Mwaka 1980 nilikuwa namba nane wa Kurugenzi Arusha, tulicheza mechi na Morani ya Arusha, nikiwa naambaa na mpira kwenda kufunga mchezaji wa Morani anaitwa King’ang’a alinichezea rafu mbaya.
“Nilipata maumivu makali ya goti ingawa kwa miaka ile sikupata matibabu ya maana, na ndiyo ukawa mwisho wangu wa kucheza soka, ila rafiki yangu mmoja alinishauri niingie kwenye ukocha na mimi nikakubali,” anasema Mwamaja.
Alipoambiwa goti lake limesagika
“Licha ya kuingia kwenye ukocha bado sikuwa na furaha kutokana na maumivu niliyokuwa nayapata kwani kuna wakati goti linaniuma hata wiki nzima mfululizo na inapotokea natumia dawa za maumivu linatulia, lakini baada ya muda linaanza tena kuuma”.
Aliongeza; “Mwaka jana nilienda kupima majibu niliyopata yanilisikitisha kwani niliambiwa goti langu la kushoto limesagika hivyo tiba pekee ni kwenda India kufanyiwa operesheni na kuwekewa kifaa bandia kitakachonisaida kupunguza maumivu ninayopata, hata hivyo nilishindwa kwenda India kwa sababu nilikosa fedha,” anasema Mwamaja.
Anasema tatizo hilo halitokani na uzito mkubwa kilo 110 alizonazo.
Mali kauli ilivyomtibulia usajili wa Ngassa
“Nikiwa kocha wa Ruvu Shooting kipindi tupo Daraja la Kwanza tulicheza mechi yetu ya mwisho Shinyanga, mechi ambayo ilitupandisha kucheza Ligi Kuu, huko ndipo nilimuona Mrisho Ngassa na Mwinyi Kazimoto ambao walikuwa wakichezea timu pinzani,” anasema Mwamaja.
Anasema alivutiwa na uchezaji na umri wao mdogo hivyo kupendekeza wasajiliwe kwenye kikosi chake.
“Kwa Ngassa tuligonga mwamba kwa kuwa tuliingia na kigezo kwamba atapata ajira ila yeye alitaka fedha ambazo hatukuwa nazo huku Kazimoto akikubali kuajiriwa hivyo tukamsajili,” anasema Mwamaja baba wa watoto watano.

Post a Comment

Previous Post Next Post