Mwanafunzi jela miaka 30 kwa ubakaji

MWANAFUNZI mmoja wa sekondari ya Hunyari, Wilaya hapa, Mkoa wa Mara, amehukumiwa kwenda jela miaka 30 na kuchapwa viboko 12 na Mahakama ya Wilaya hiyo kwa kosa la kumbaka mwanafunzi wa shule ya msingi (18) jina linahifadhiwa.
Akimsomea shitaka lake, mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Safina Simufukwe, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Masoad Mohamed, alisema mshitakiwa huyo mwenye umri wa miaka 24 aliyekuwa anasoma kidato cha nne katika shule hiyo alitenda kosa hilo mnamo Novemba 17, mwaka huu majira ya saa 4:00 usiku katika kijiji cha Sarawe.
Mohamed alisema mshitakiwa ni mwanafunzi anayesubiri matokeo ya kidato cha nne baada ya kufanya mtihani mwaka huu, alimbaka mwanafunzi huyo anayesoma darasa la saba katika shule ya msingi Sarawe, baada ya kumfungia ndani ya chumba chake nyumbani kwao kwa muda wa siku mbili mfululizo.
Alisema kabla ya mwanafunzi huyo kukamatwa, viongozi wa kijiji hicho walipata taarifa ya mwanafunzi huyo kumfungia ndani mwanafunzi mwenzake na kumbaka kwa siku hizo.
Aliongeza kuwa viongozi wa kijiji hicho wakiwa na wananchi walikwenda katika eneo la tukio majira ya usiku na kumkuta mwanafunzi huyo akimfanyia kitendo hicho mwenzake na ndipo alikamatwa na kupelekwa katika kituo cha polisi Nyamuswa.
Baada ya kusomewa shitaka lake mwanafunzi huyo alikiri kufanya kosa hilo, huku akidai kuwa mwanafunzi huyo wa darasa la saba ni mpenzi wake wa siku nyingi na kwamba anaomba asamehewe na Mahakama hiyo.
Kutokana na kukiri kosa hilo Hakimu Simufukwe alimtia hatiani na kumuhuku kifungo cha miaka 30 jela pamoja na kuchapwa viboko 12, ili liwe fundisho kwake na kwa wanafunzi wengine, pamoja  na watu wenye wenye tabia au nia ya kutenda kosa ya ubakaji.

Post a Comment

أحدث أقدم