![Serikali yaipongeza Tusiime kuingia kumi bora kitaifa Serikali yaipongeza Tusiime kuingia kumi bora kitaifa](http://freemedia.co.tz/daima/wp-content/uploads/2014/11/tusiime-300x169.jpg)
SERIKALI imeipongeza
shule ya Tusiime kwa kuwa shule pekee kutoka Mkoa wa Dar es salaam
iliyoingia kwenye kumi bora kitaifa na kufaulisha wafunzi wote 168 kwa
alama A na kuongoza katika mkoa wa Dar es salaam na wilaya ya Ilala.
Pongezi hizo zilitolewa mwishoni mwa wiki na Kaimu Ofisa Elimu Mkoa
wa Dar es Salaam, Bernadetha Thomas, wakati wa mahafali ya kumaliza
shule ya msingi na awali Tusiime Tabata jijini Dar es Salaam, ambayo
ndiyo pekee katika shule kumi bora yenye wanafunzi zaidi ya 100 kwenye
matokeo ya darasa la saba mwaka huu.
“Nasema hivyo kwa sababu shule hii ni miongoni mwa shule bora nchini,
na kama mnavyojua matokeo ya mitihani ya taifa yanadhihirisha
hili…tunapozungumzia mafanikio ya shule hii, tunamaanisha juhudi zenu
wazazi na wafanyakazi wote wa Tusiime.
“ Nimefarijika sana kusikia uongozi wa shule unajali maslahi ya
wafanyakazi, hilo ni jambo jema kwa sababu wao ndio wazalishaji wakuu na
ndio watenda kazi, kujali maslahi yao na kuwapa motisha ni kuongeza
tija na hatimaye ufanisi….kuna baadhi ya wawekezaji katika sekta ya
elimu hujali zaidi faida bila kujali maslahi ya mzalishaji wa faida
hiyo,” alisema.
Aidha aliwapongeza wamiliki wa shule hiyo kwa uamuzi wao wa busara
kuwekeza kwenye elimu na kwamba uamuzi wao umepanua wigo wa fursa za
elimu nchini na kuchangia ukuaji.
Awali katika risala yake, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Philbert Simon,
alisema shule yake imetimiza miaka 15 yenye mafanikio katika
taaluma na nje ya taaluma na aliahidi wataendelea kufanya hivyo kwa
kuongeza bidii na maarifa zaidi katika kazi zao ili kuzalisha raia
mahiri na wenye tija kwa taifa.
Alisema mafanikio yao yametokana na kuwa na timu nzuri ya wanataaluma wanaokidhi viwango na kujituma .
“Katika kutekeleza matokeo makubwa sasa (BRN) shule yetu imesimamia
kwenye rangi ya kijani ambayo ndio kielelezo cha ushindi wa juu kabisa.
Tutatumia raslimali na uwezo wetu wote tuliojaliwa kuhakikisha
tunailinda nafasi hiyo,” alisema Simon.
Post a Comment