Ukawa wafichua njama

Dodoma. Wakati kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) ikianza kupitia ripoti ya IPTL kuhusu uchunguzi wa ufisadi katika Akaunti ya Tegeta Escrow, wabunge wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), umedai kwamba kuna mikakati imeandaliwa kuzima ripoti hiyo kusomwa na kujadiliwa bungeni.
Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia alisema jana kwamba moja ya mikakati hiyo ni madai ya kuwapo barua ya Mahakama kuzuia mjadala huo akisema mkakati huo unatokana na ukubwa wa kashfa na jinsi inavyowahusisha viongozi waandamizi serikalini.
Mbatia aliyeambatana na kundi kubwa la wabunge kutoka Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi, alisema: “Iko mikakati na mbinu za kila aina kulihujumu Bunge lisisimamie fedha za walipakodi, ndiyo maana kuna danadana na tuna taarifa za kuwapo barua kutoka mahakamani kuzuia jambo hilo lisijadiliwe bungeni kwa madai eti kuna kesi.
“Mahakama haiwezi kuingilia shughuli za Bunge, inatia wasiwasi kwa kuwa Ofisi ya Bunge nayo imekuwa na danadana kila siku kwa kubadilisha badilisha ratiba wakati sisi tunataka hawa waliohusika kwenye kashfa hii wachukuliwe hatua.”
Pia, alisema kuna taarifa kwamba Serikali inadai haina fedha, ikitaka kufupisha Bunge na suala hilo lisijadiliwe sasa hivi.
Mbunge wa Mkanyageni (CUF), Mohammed Mnyaa alisema: “Serikali inategesha tegesha tu mambo bungeni na ndiyo maana leo (jana) wameahirisha Bunge hadi kesho (leo) bila sababu za msingi, wanafinya muda wa sisi kujadili sakata hili,” alisema Mnyaa.
Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisema escrow ni kama ilivyokuwa kashfa ya Richmond ambayo iliwang’oa wahusika wakuu bungeni, hivyo haiwezekani isijadiliwe bungeni kwa madai kwamba Mahakama imezuia...
“Hakuna utaratibu kama huo wa Mahakama kuelekeza Bunge kitu gani kifanyike na gani kisifanyike pia hata Katiba hairuhusu hilo.”
Lissu alishangazwa na Naibu Spika, Job Ndugai kuahirisha Bunge jana hadi leo kwa madai kuwa yeye (Lissu) alikuwa hajakamilisha taarifa ya upinzani kwenye muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2014 akidai kuwa huo ni upotezaji wa muda.
“Nilimwomba Naibu Spika kuwa aahirishe muswada huo hadi kesho kwa kuwa ulikuwa umepangwa tarehe 25 lakini ghafla ukabadilishwa na mimi sikuwapo kwa muda wote huo. Sikuomba aahirishe Bunge nilimwomba aahirishe muswada tu,” alisema Lissu.
Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe alisema naye amesikia kuwapo barua ya Mahakama kuzuia mjadala huo na kusema kama ni kweli, halitakuwa sahihi.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara katika Operesheni Delete CCM mjini Dodoma jana, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema si Waziri Mkuu wala Jaji Mkuu anayeweza kuuzima mjadala wa escrow bungeni.
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post