Vikosi vya Somalia vyazuia mipango ya al-Shabaab huko Mogadishu

Na Fuad Ahmed, Mogadishu

Vikosi vya usalama vya Somalia vimekuwa vikifanya operesheni ya saa 24 huko Mogadishu tangia mwanzoni mwa mwezi wa Novemba, vikizuia mashambulio yapatayo 20 na kukamata dazeni za viongozi wa al-Shabaab na wapiganaji zaidi ya 20 wa al-Shabaab, kwa mujibu wa Wizara ya Usalama ya Taifa.

Vikosi vya usalama vya Somalia na raia wakiwa wamesimama karibu na eneo ambalo gari lililolipuliwa kwa bomu katika barabara ya Maka al-Mukarama huko Mogadishu tarehe 16 Novemba, 2014. [Abdifitah Hashi Nor/AFP]

Al-Shabaab ilikuwa imepanga shambulio la kujitoa muhanga likilenga wakaazi wa wilaya ya Dharkenley waliokuwa wakienda kwenye sala ya alfajiri Ijumaa iliyopita (tarehe 14 Novemba), alisema msemaji wa wizara Mohamed Yusuf Osman, lakini vikosi vya usalama viliweza kuzuia shambulio hilo.

"Tuliwakamata watu watano ambao walikuwa wamejiandaa kutekeleza ulipuaji wa bomu la kujitoa muhanga na mtu ambaye alikuwa amewapa hifadhi, [na kunyang'anya] fulana nne za mlipuko ambazo zilikuwa kwenye mikoba ya akina mama," aliiambia Sabahi.

"Wote walikuwa wanataka kulipua bomu la kujitoa muhanga dhidi ya umma Ijumaa asubuhi, lakini tuliweza kuzuia hilo kutokana na taarifa tulizopokea kutoka kwa raia wa wilaya ya Dharkenley huko Mogadishu," alisema.

Wakati wa operesheni hii, vikosi vya usalama vilikamata silaha na magari matano ambayo al-Shabaab ilikuwa ikiyatumia kupiga risasi huku wakiendesha, likiwemo gari lililotumiwa katika mauaji ya sababu za kisiasa ya watunga sheria watano wa Somalia, akiwemo Saado Ali Warsame.

"Magari hayo pia yalitumiwa kufanya utoroshaji na uuaji wa raia kadhaa," Osman alisema.

"Serikali pia imechukua nyumba nne na gereji tatu ambazo zilikuwa zinatumiwa kama ngome ya kuandalia milipuko," alisema.


Osman aliwaomba wakaazi wa Mogadishu kuwa watulivu na kuwa na tahadhari kuhusu mahali wanakoegesha magari yao ili wahusika wa al-Shabaab wasiweke milipuko kwenye magari yao.

"Usalama kamili sio kitu ambacho kinaweza kufanikiwa [mara moja]," alisema, akiuomba umma kutokata tamaa kwa mashambulio ya mara kwa mara ya kikundi.

"Kinachotokea sasa ni kwamba al-Shabaab wanatapatapa kwa kukata tamaa kwa kushindwa kufanikisha malengo yake baada ya kushindwa [na Somalia na vikosi washirika]," Osman alisema. "Sasa, wanataka kuwaumiza raia na kusababisha maangamizi ili waweze kusema, 'Bado tuko hapa na tumesababisha mlipuko'."

"Lakini matatizo na uharibifu ambao umeletwa na al-Shabaab ni mkubwa kuliko hilo, hivyo hebu tusizingatie kufedheheka na tuendelee kuunga mkono mfumo wa usalama," alisema.

Hatua za ziada za usalama zinatakiwa
Kanali mstaafu wa jeshi la taifa la Somalia Dahir Timaadde alikaribisha operesheni ya usalama ya hivi karibuni lakini alisema bado kuna dosari za usalama ambazo zinahitaji kushughulikiwa.

"Vikosi vya usalama haviko katika hali inayofanana kama vilivyokuwa miaka mitatu iliyopita wakati vilipokuwa na uhaba wa vifaa," aliiambia Sabahi. "Hata hivyo, bado inaonekana kuna masuala mengi kutokana na ukweli kwamba mauaji bado yanatokea kwenye makutano ya barabara kuu kwa sababu hakuna vikosi vya usalama."

Serikali ya Somalia inapaswa kuweka magari ya polisi katika kila makutano huko Mogadishu ili kushughulikia dharura kwa wakati, Timaadde alisema.

"Tunaendelea kusikia kwamba makundi katika magari yamewaua watu wanaofanya kazi na serikali na walifanikiwa kukimbia tukio hilo la uhalifu," alisema. "Hilo linaonyesha kukosekana kwa uwezo wa vikosi vya usalama. Serikali inatakiwa kuja na mpango kamili wa kuzuia majanga hayo."

"Wakati ninajua kwamba usalama hauko thabiti kama ulivyopaswa kuwa, vikosi vya usalama vinastahili sifa yetu kwa kuwa wameshiriki katika jitihada za kuhakikisha usalama," alisema mkaazi wa Mogadishu mwenye umri wa miaka 25 Maryam Mohamud, ambaye alisoma utawala wa umma katika Chuo Kikuu cha Somalia.

"Tunapaswa kushirikiana nao kwa moyo wote ili kutokomeza ugaidi," aliiambia Sabahi, akitoa wito kwa raia kuongeza msaada wao kwa vikosi vya usalama ili jiji liishi kwa amani.

Mohamud pia alitoa wito kwa serikali kuhamasisha wapiganaji wa al-Shabaab kubadilika wenyewe chini ya programu ya msamaha na kuwahakikishia usalama wao ili waamini jitihada hizo.

"Serikali inapaswa kuendesha kampeni ya uelimishaji inayoendelea ili kuwafanya watu wanaotaka kubadilika wenyewe kujua kuwa hawatakabiliwa na matatizo yoyote," alisema. "Serikali inapaswa pia kuongeza idadi ya vituo vya mabadiliko ili wenye itikadi ya msimamo mkali wangebadilishwa fikra [kuamini] wameacha kutoka katika mawazo yao."

Vijana pia wanapaswa kupewa mafunzo ya ufundi ili kwamba waweze kutafuta kazi za kuwasaidia wao wenyewe na kutoamuliwa kujiunga na al-Shabaab kwa kuahidiwa fedha, alisema Mohamud, akiwaomba washirika wa kimataifa wa Somalia na mashirika ya msaada kuunga mkono jitihada hizo.

Post a Comment

أحدث أقدم