Wakati umefika wa kubadilisha mfumo wa elimu

Matokeo ya mitihani ya darasa la saba imetoka, tumejisifu kuwa tumefaulisha zaidi ya nusu ya wanafunzi waliofanya mtihani huo, lakini tunasahau kuwa waliofeli pia ni karibu ya nusu kwani waliofaulu ni 451,392 na waliofeli ni 356,693.
Hiyo haiakisi jitihada za serikali za Matokeo Makubwa Sasa (BRN), kwani hayo ni matokeo ya wastani tu wala si makubwa.
Tunajitahidi kuanzisha mipango na mikakati ya kufufua elimu, tulikuwa na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Msingi (MMEM), Elimu ya Msingi kwa Wote (Universal Primary Education -UPE) na mipango mingine mingi tu, lakini kimsingi haijasaidia kuinua kiwango cha elimu nchini.
Watanzania tunajitahidi kuweka dawa ya kidonda katika kidonda ambacho kimeota gaga (gamba), dawa zozote tutakazoziweka juu ya gaga ni dhahiri kuwa hazitaponyesha kidonda kwa sababu kipo kitu kinachozuia dawa isifike kwenye kidonda.
Ili kutatua tatizo hilo tunapaswa kuliondoa gaga kwanza na gaga hili la elimu ni mfumo. Mfumo wetu wa elimu bado ni wa mwaka 1947, si mfumo kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania, bado ni mfumo wa kikoloni uliokuwa na dhamira ya kumwelimisha Mwafrika kusoma na kuandika ili aweze kutekeleza kazi alizopangiwa kama vile ukarani, upolisi na ualimu.
Miaka 53 sasa tokea tupate Uhuru, tumekuwa tunauweka viraka tu mfumo wetu wa elimu badala ya kuufumua na kuunda upya kutokana na mahitaji na matakwa yetu na matakwa ya maendeleo ya karne tuliyonayo.
Bahati mbaya zaidi hata huo mfumo tulionao na ambao tumeuzoea tunashindwa kuutendea haki kwa sababu ya kuwa na miundombinu ya elimu iliyo dhaifu na hafifu.
Tunalifanya suala la elimu kama la kisiasa badala ya kuwa la kitaaluma na kimkakati, tunapaswa tuweke vipaumbele vyetu vyote katika elimu kama tunataka kuondokana na hali hii ya mkwamo wa kimaendeleo tulionao.
Inashangaza kuona kwamba kila mwaka serikali yetu inaainisha vipaumbele kati ya saba na nane katika bajeti ya Serikali. Haya ni makosa makubwa kwani kwa kuwa tuna rasilimali chache, tukiwa na vipaumbele vingi maana yake tumekusudia kugawana umaskini.
Zipo nchi ambazo katika miaka ya 60 uchumi wake ulikuwa sawa na uchumi wa Tanzania, hivi leo zinashangaza dunia kwa jinsi uchumi wake unavyopaa. Nchi kama Korea ya Kusini, Malaysia na Singapore (kwa kuzitaja chache) ni nchi za kupigiwa mfano, zimeweka sera na mikakati ya kuinua uchumi sio tu wa nchi bali hata wa wananchi wake na silaha kubwa waliyoitumia ni elimu.
Kwanza walijivua kutokana na kamba za ukoloni, waliondosha mfumo kandamizi wa elimu na kuweka mfumo huru kwa wananchi wake na kufundisha kwa kutumia lugha wanayoielewa, lugha yao mama na wala si Kiingereza, Kifaransa, Kiitaliano au Kireno.
Sisi huku kwetu uamuzi wa kutumia Kiswahili kama lugha ya kufundishia umegeuzwa uamuzi wa kisiasa. Kwetu sisi bado tumebaki na kasumba za kikoloni, usipojua Kiingereza hujasoma vyema na hata fursa za kuajiriwa huwa chache. Bado tunakubali kubaki na tongotongo za ukoloni.

Post a Comment

أحدث أقدم