MZIMU
wa kumshambulia aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba
Jaji mstaafu, Joseph Warioba umeibukia tena bungeni baada ya Mbunge wa
Rombo Joseph Selasini (CHADEMA) kuhoji kwanini ameondolewa walinzi na
Serikali.
Katika swali hilo, mbunge huyo alitaka Serikali ieleze ina mkakati
gani wa kuimalisha ulinzi kwa wastaafu waliokuwa viongozi wakuu wa
taifa, akiwamo Jaji Warioba ambaye amepata kuwa Waziri Mkuu.
Selasini aliihoji serikali ina mikakati gani ya kuwalinda wazee hao
mbao walikuwa walilitumikia taifa, lakini baadhi yao hivi sasa
wanatishiwa maisha na kudhalilishwa.
“Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tumeona jinsi mzee wetu, Jaji
Joseph Warioba alivyodhalilishwa kwa kutaka kupigwa na vijana wa kihuni
jijini Dar es Salaam kwanini hana ulinzi au ndio ameondolewa ulinzi?
alihoji Selasini.
Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi), Celina
Kombani alisema viongozi wote wastaafu wanalindwa na wanatunzwa na
serikali.
Alisema serikali ina viongozi wastaafu 13 ambao wamewahi kuwa marais
na mawaziri wakuu na kwamba wote wana walinzi na wanatunzwa na serikali
kwa mujibu wa sheria.
“Mfano ni hapa bungeni, si unamwona Mheshimiwa Lowassa ana walinzi
wawili na hao wengine, wote wana walinzi na wanatunzwa vizuri na
serikali, hata Jaji Warioba anao walinzi labda kama aliwaacha siku
hiyo,” alisema Kombani.
Majibu hayo, yalimwinua tena Seleasini na kuomba mwongozo wa Spika kuonyesha kutoridhishwa na majibu mepesi ya Waziri Kombani.
Selasini alisema Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi aliwahi kupigwa kofi
hadharani, Rais Kikwete alishawahi kuvamiwa jukwaani kule Mwanza na
kwamba juzi Watanzania wameona jinsi Jaji Warioba alivyofanyiwa.
“Ukiacha mbali wazee hao kushambuliwa, Mama Maria Nyerere alishawahi
kulalamika hana maji, kule Butiama nyumbani kwa baba wa Taifa hakuna
maji, chooni unaingia na ndoo na kopo, pia Msasani maji yamekatwa, hata
jenereta lililopo ni bovu la mwaka sabini, lakini Waziri anakuja na
majibu mepesi.
“Kama hilo Jina la Warioba linawauma wengine vifuani mwenu hamtaki
kulisikia basi vumilieni lakini suala la msingi hapa ni usalama wa
maisha ya viongozi wetu wastaafu wala hakulengwa mmoja kama waziri
alivyojibu hapa,” Mheshimiwa Naibu Spika naomba mwongozo wako.
Awali katika swali la msingi la Selasini alitaka kujua serikali ina
wazee wangapi wa kuanzia miaka sitini na kuendelea na kama kuna mkakati
wa kuwapa huduma mbalimbali kama vile chakula, malazi, matibabu na
kadharika.
Aidha alitaka kujua kama serikali haioni umuhimu wa kuanzisha kitengo
maalum cha kuwatambua, kuwahudumia na kuwaenzi kama ilivyo kwa watoto
na akina mama.
- Tanzania Daima

إرسال تعليق