Wizara ya Ardhi inaongoza kwa uzembe – Mbunge

MBUNGE wa Gando, Khalifa Suleiman Khalifa (CUF), amesema kuwa kati ya Wizara ambazo zinalalamikiwa kwa uzembe ni Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Khalifa, aliyasema hayo bungeni jana alipokuwa akiuliza swali la nyongeza kwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, George Simbachawene.
Mbunge huyo, alisema kuwa Wizara hiyo imekuwa ikilalamikiwa na Wananchi kwa uzembe kutokana na utendaji usioridhisha, jambo ambalo si jema.
Aidha, Mbunge huyo alitaka kujua kama Wizara hiyo imekuwa ikiwakagua Watumishi wake kwa kuangalia utendaji wao wa kazi na kama wamebaini mapungufu, je wanatoa taarifa kwa Rais ili waweze kuchukuliwa hatua stahiki?
Pia, alitaka kujua hadi sasa kuna Wafanyakazi wangapi wa Wizara ya Ardhi ambao wamefukuzwa kazi kutokana na utendaji mbovu wa kazi.
Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri George Simbachawene alisema kuwa sekta ya Ardhi ni pana na imekuwa ikikabiliwa na matatizo makubwa, lakini pia ina Sheria zake.
Alisema kuwa, kutokana na upana huo wa sekta ya ardhi sheria zake zimekuwa na migongano mingi licha ya kuwepo kwa juhudi katika kuzitatua.
“Kila kukicha tumekuwa tukichukua hatua ambapo kila baada ya miezi mitatu, tumekuwa tukimsimamisha mfanyakazi mmoja wa Wizara ya Ardhi kutokana na makosa mbalimbali,” alisema.
Katika swali la msingi ambalo liliulizwa na Mbunge wa Tanga Mjini, Omar Nundu (CCM), aliyetaka kujua je ni lini Serikali itatengua umiliki wa mashamba ya mkonge ya Mkoa wa Tanga ili wananchi hao waishi maisha ya amani.
Pia, alihoji Serikali inachukua hatua gani kuzuia tabia ya wamiliki wa mashamba hayo kuuza kwa watu wengine endapo yatagunulika kama yametekelezwa.
Akijibu maswali hayo, Simbachawene alisema kuwa Wizara yake ilishawasilisha mapendekezo kwa Rais Jakaya Kikwete, kubatilisha miliki za mashamba kwa Mkoa wa Tanga ambayo yametelekezwa kwa muda mrefu ili zibatilishe.
“Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu Mheshimiwa Spika kuwa, Mheshimiwa Rais ameridhia miliki za mashamba ya Bombwera, Kihuhwi, Sagulas, Lewa, Kwafungo na Geigliyz/Kilapuka zibatilishwe ili haimaye yagawiwe kwa wananchi,” alisema Naibu Waziri huyo.

Post a Comment

Previous Post Next Post