Wafanyakazi wapya katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH),
wamelalamikia kutolipwa mishahara kwa miezi minne sasa, huku uongozi
ukishindwa kuwapa majibu ya ufumbuzi wa tatizo hilo.
Wafanyakazi hao zaidi ya 50 walioajiriwa tangu
mwezi wa nane mwaka huu, waliliambia gazeti hili kwa nyakati tofauti
kuwa hawajalipwa hata shilingi moja tangu walipoajiriwa.
Walilalama kwamba kilichofanyika hadi sasa ni
baadhi yao kupewa namba za hundi, lakini walipokwenda kuangalia kwenye
akaunti zao hawakukuta kitu.
“Sisi tunashangaa kukaa muda wote huu bila kulipwa
hata senti tano, huku tukipangiwa majukumu. Kama tumeajiriwa na
Serikali, si inakuwa imeshatenga bajeti yetu kabisa, kwa nini tunapata
usumbufu huu? Haki ipo wapi? ” alilalama mmoja wa wafanyakazi hao
wanaofanya kazi idara mbalimbali wakiwamo wauguzi, watunza kumbukumbu na
masijala.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano cha Hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha alikiri kuwapo kwa hali hiyo.
Hata hivyo alisema wafanyakazi wenye madai hayo ni
10 na wataanza kulipwa mwisho wa mwezi huu. “Ni kweli hawajalipwa
mishahara tangu walipoajiriwa Agosti mwaka huu kwa sababu majina yao
yalikuwa hayajaingizwa kwenye utaratibu wa malipo wa Serikali,”alisema.
Post a Comment