Jezi ya Okwi yazua... vurugu

Straika wa Simba, Emmanuel Okwi.
Sweetbert Lukonge na Wilbert Molandi SOKA la Bongo kweli balaa! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya juzi Jumamosi, Kocha Mkuu wa Yanga, Mbrazili, Marcio Maximo kutaka kurusha makonde uwanjani baada ya kushushiwa matusi na makomandoo wawili wa klabu hiyo.
Kisa kikubwa cha tafrani hiyo, kilitokana na kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima, kubadilishana jezi na straika wa Simba, Emmanuel Okwi, hatua ambayo iliwakera sana makomandoo wa Yanga.
Tukio hilo lililokuwa la kusikitisha na kushangaza lilitokea baada ya kumalizika kwa mechi ya Nani Mtani Jembe 2 dhidi ya Simba baada ya kushuhudia kikosi chake kikilala kwa mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar.
Baada ya mechi hiyo, Makomandoo ya Yanga walijipanga mstari katika njia ya wachezaji na viongozi kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo uwanjani hapo, ambapo kazi yao kubwa ilikuwa ni kuwazuia waandishi wa habari wasizungumze jambo lolote na wachezaji hao.
Makomandoo hao waliendelea kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa lakini mwisho walikumbana na kizingiti kutoka kwa kiungo wa timu hiyo, Mnyarwanda, Haruna Niyonzima ambaye anatambua vilivyo kazi yake.
Niyonzima aliwagomea makomandoo hao wasimshurutishe kama mtoto wakati alipokuwa akizungumza na gazeti hili akitoa tathmini ya mchezo huo kama sheria za soka zinavyoruhusu, hivyo kuwaambia hawana haki ya kumzuia asiongee na waandishi wa habari.
Kauli hiyo ya Niyonzima iliwakera makomamdoo wawili waliokuwa wakimshurutisha na kuonekana kupandwa na jazba na kuanza kumtolea matusi ya nguoni Niyonzima kuhusu mama mzazi wake, jambo ambalo pia lilimkasirisha kiungo hiyo na kutokwa na machozi.
Makomandoo hao waliofahamika kwa jina moja moja, Said na Carlos, waliendelea kumshambulia nyota huyo kwa matusi mazito mpaka alipoingia kwenye chumba cha kubadilishia nguo, ndipo Maximo aliposikia matusi yale na hali halisi ilivyokuwa, akatahamaki na kutaka kumfuata Said ili waonyeshane umwamba.
Maximo alipandwa na jazba na kukurupuka kutoka chumbani na kutaka kwenda kupambana na makomandoo hao ambao vinywa vyao vilitawaliwa na matusi mazito na yasiyovumilika kwa binadamu yeyote.
Hata hivyo, baadhi ya viongozi wa benchi la ufundi wa timu hiyo wakiongozwa na kocha msaidizi, Mbrazili, Leonardo Neiva pamoja na daktari Juma Sufiani, walifanya kazi ya ziada kumdhibiti Maximo asitoke nje ya chumba hicho kwenda kupambana na watu hao.
Tukio hilo pia, lilishuhudiwa live na viongozi wengine akiwemo mwenyekiti wa kamati ya vijana, Bakili Makere pamoja na ofisa habari wao, Baraka Kizuguto ambaye muda wote alikuwa kimya huku akitikisa kichwa kuashiria kuhuzunishwa na nidhamu mbovu iliyoonyeshwa na watu wao.
Hata hivyo Kizuguto hakuwa tayari kulizungumzia suala hilo lakini kocha wa timu hiyo, Shadrack Nsajigwa, alisema kuwa kitendo hicho kilichofanywa na makomandoo hao si cha kiungwana.
Kwa upande wake Niyonzima aliliambia Championi Jumatatu kuwa, kitendo hicho hakijamfurahisha hata kidogo kwani kufungwa ni jambo la kawaida, hivyo anashangaa kuona makomandoo hao wanamshambulia kwa matusi ikiwa ni pamoja na kumzuia kuzungumza na waandishi wa habari wakati wao siyo waliomuajiri.
Licha ya viongozi kusawazisha hali ile, Said aliendelea kumuandama Niyonzima kwa matusi na kumwambia kuwa yeye ni mkimbizi na muda wowote ataondolewa Yanga na hana lolote anajipendekeza tu kuwa ndani ya Yanga.
Baadaye ilikuja kubainika kuwa, kisa kikubwa cha makomandoo hao kukasirika kupita kawaida kilitokana na Niyonzima kubadilishana jezi na Emmanuel Okwi na kuwapongeza wachezaji wa Simba baada ya mchezo.
Akiwa na jezi aliyopewa na Okwi, Niyonzima alivamiwa na makamandoo wa Yanga na kumhoji kwa nini alikubali kubadilishana jezi na Okwi, pia kwa nini apeane mikono na wachezaji wa Simba baada ya mechi hiyo kumalizika.
Makomandoo hao pia waliwavamia wachezaji ndani ya vyumba vya kubadilishia nguo na kuanza kuwabwatukia wakidai hawajitumi, tukio ambalo Nsajigwa ameliponda vikali akisema halijengi bali linabomoa.

Post a Comment

أحدث أقدم