Mabaunsa Mwanza watwangana makonde na wafuasi wa Chadema.

Kituo cha kupigia kura kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa, vitongoji na vijiji cha minazi mitatu kata ya kitangiri manispaa ya ilemela leo asubuhi kiligeuka uwanja wa masumbwi baada ya mabaunsa kadhaa wa meya wa manispaa ya ilemela Bw. Henry matata kutwangana makonde hadharani na wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo (Chadema), huku baadhi ya vituo vya kupigia kura wilayani humo vikikabiliwa na mapungufu ya vifaa.
ITV imefika katika kituo hicho majira ya saa 5 asubuhi na kukuta ugomvi ukiwa umepamba moto huku baadhi ya wapiga kura wakimlalamikia diwani wa kata hiyo Bw. Henry Matata ambaye pia ni mstahiki meya wa manispaa ya Ilemela kuchochea vurugu hizo kwa kuwatumia mabaunsa wake kuwashambulia kwa kipigo vijana wa Chadema.
 
Alipoulizwa kuhusiana na vurugu hizo, meya huyo wa manispaa ya Ilemela Bw. Henry Matata amedai kuwa chanzo cha vurugu hizo ni kutokana na baadhi ya wafuasi wa Chadema kuanza kuwazuia baadhi ya akinamama kupiga kura.
 
Msimamizi wa uchaguzi huo, ambaye pia ni kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya manispaa ya Ilemela Justin Lukaza anaeleza baadhi ya changamoto zilizojitokeza katika zoezi hilo la uchaguzi.
 
Katika kituo cha kupigia kura cha jiwe kuu manispaa ya Ilemela, hadi inatimu saa 6 mchana zoezi la upigaji kura lilikuwa katika hali ya sintofahamu hali iliyosababisha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wapiga kura, huku katika kituo cha Kitangiri ‘B’ orodha ya majina ya wapiga kura iliyokuwa imebandikwa katika ofisi ya afisa mtendaji wa kata ya kitangiri ilikuwa imefutika.
 
Halmashauri ya manispaa ya Ilemela ina vituo 262 vya kupigia kura na mitaa 172 ambayo inawaniwa na wagombea wa vyama saba vya CCM, Chadema, CUF, TLP, UDP, ACT na ADC na habari zilizotufikia hivi punde kutoka wilayani Sengerema zinasema kuwa uchaguzi huo katika jimbo la Buchosa umehairishwa hadi jumamosi ijayo kufuatia kukumbwa na dosari kadhaa, ikiwemo upungufu wa vifaa vya kupigia kura na viashiria vya uvunjifu wa amani.
- ITV

Post a Comment

Previous Post Next Post