Askari waliosababisha kifo Serengeti kubanwa


Serengeti. Polisi mkoani Mara imesema itawachukulia hatua askari watakaobainika kuhusu katika kifo cha Samson Nyakiha (70) baada ya uongozi wa jeshi hilo kukutana na ndugu wa marehemu waliotelekeza maiti katika Kituo cha Polisi cha Wilaya.
Kamanda wa upelelezi wa makosa ya jinai wa mkoa, RCO Rogathe Mlasani alitoa ahadi hiyo katika kikao cha pamoja cha ndugu na uongozi wa polisi wa Wilaya ya Serengeti na kisha kutangaza kwa wananchi waliokuwa wamekusanyika katika kituo hicho tangu Alhamisi kusubiri hatma ya suala hilo.
Katika tukio hilo, mwili wa Nyakiha aliyefia Hospitali ya Rufaa ya Bugando ulichukuliwa na ndugu ambao waliupeleka kituo hicho cha polisi na kuutekeleza, wakidai ndugu yao aliuawa kutokana na kupigwa na askari.
RCO Mlasani alisema tukio hilo si la kawaida kwa kuwa limesababisha kupoteza uhai wa mtu na haliwezi kuvumiliwa kwa kuwa limekiuka misingi ya haki za binadamu.
Aliwaomba wananchi wawe watulivu wakubali kuchukua mwili wa marehemu wakazike.
“Naomba mliamini Jeshi la Polisi kwa kitendo kama hiki hakuna atakayelindwa, wote watachukuliwa hatua kulingana na makosa waliyoyatenda. Kwa hili hatutamlinda mtu maana kila mmoja anajua mipaka ya kazi yake,” alisema.
RCO alisema kuanzia sasa jalada la uchunguzi wa tukio hilo analichukua yeye na litakuwa la kifo cha shaka na upelelezi huo umehamishiwa ofisi yake.
Alisema hatua za kipolisi zinaanza haraka kwa askari wa Shirika la Hifadhi ya Taifa (Tanapa) na polisi waliohusika na wakati huo taarifa ya kifo itakuwa inasubiriwa na baada ya hapo hatua zaidi zitachukuliwa kwa watakaothibitika kuhusika bila kujali nyadhifa zao.
Ndugu wa marehemu wakiongozwa na Wakili Stephen Magoiga, walimtaka RCO kutoa taarifa ndani ya wiki moja kuhusu hatua zitakazokuwa zimechukuliwa na watu gani wamehusika.
Nyamaisa Damas (40), mke mdogo wa marehemu alisema Novemba 16, 2014 saa 12:00 asubuhi kundi la askari lilimvamia mumewe na kufanya upekuzi na kuchukua silaha na risasi alizokuwa anamiliki kihalali na wakachukua simu yake.
Alisema askari hao waliondoka naye akiwa mzima na baadaye ghafla alisikia mumewe amelazwa hospitali na hajitambui.
Hata hivyo, kwenye jalada Mug/Ir/31/74/2014 alilofunguliwa Nyakiha linaeleza kuwa alikutwa na ngozi tano za nyumbu, mavi ya tembo, bangi, bunduki aina ya shortgun na risasi zake. Alieleza kuwa anamiliki bunduki kihalali na kwamba shuhuda ni mkewe, lakini polisi walikataa maelezo hayo.

Post a Comment

أحدث أقدم