Dar es Salaam. Hatimaye Rais Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko
13 kwenye Baraza la Mawaziri yaliyohusisha mawaziri nane, manaibu
watano, wakiwamo wapya wawili, ikiwa ni siku mbili kabla ya kuanza kwa
Bunge, na ndani ya saa 48 kama gazeti hili lilivyoripoti Ijumaa
iliyopita.
Rais pia aliwaapisha mawaziri wote 13 akiwamo
waziri mpya wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe ambaye
alisababisha hafla hiyo kuchelewa kwa kuwa alikuwa akitokea Davos,
Uswisi.
Mabadiliko hayo, yanayoweza kuwa ya mwisho kwa
Rais Kikwete, yamefanyika ikiwa imesalia miezi sita kabla ya kuvunjwa
kwa Bunge kupisha Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba.
Rais amelazimika kufanya mabadiliko hayo baada ya
mawaziri wawili, Profesa Anna Tibaijuka na Profesa Sospeter Muhongo,
kuondoka kutokana na kuhusishwa na kashfa ya uchotwaji fedha kwenye
akaunti ya Tegeta Escrow, ambayo pia imesababisha Katibu Mkuu wa Wizara
ya Nishati na Madini, Eliackim Maswi kusimamishwa kazi, huku waziri wa
zamani wa wizara hiyo, William Ngeleja akivuliwa uenyekiti wa Kamati ya
Bunge ya Sheria.
Kwa mujibu wa mabadiliko hayo, Kikwete amewaondoa
mawaziri wawili wazoefu kutoka Ofisi ya Rais, Steven wasira na Ofisi ya
Waziri Mkuu, William Lukuvi, kuwapangia wizara nyingine, huku
akimhamishia Dk Mary Nagu kwenye Ofisi ya Rais na Jenister Mhagama
(Waziri Mkuu).
Akitangaza mabadiliko hayo jana, Katibu Mkuu
Kiongozi Ombeni Sefue alisema mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene,
ambaye alikuwa naibu wa wizara ya Nishati na Madini kuanzia mwaka 2012
hadi 2014 na ambaye hadi jana alikuwa naibu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba
na Maendeleo ya Makazi, ameteuliwa kumrithi Profesa Muhongo kwenye
wizara hiyo tata ya Nishati na Madini.
Simbachawene anakuwa waziri wa nne kushika wizara
hiyo tangu Serikali ya Awamu ya Nne iingie madarakani na anaingia wakati
Steven Masele, aliyekuwa naibu Waziri wa Nishati na Madini, akiwa
amehamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano). Nafasi ya Masele
imechukuliwa na mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage ambaye
ameteuliwa kwa mara ya kwanza.
Sefue alisema mbunge wa Ismani, William Lukuvi,
ambaye tangu mwaka 2010 amekuwa Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,
Utaratibu na Bunge), ameteuliwa kuziba nafasi ya Profesa Tibaijuka ya
uwaziri wa Kazi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Sura nyingine ngeni kwenye baraza hilo, kwa mujibu
wa Sefue, ni ya mbunge wa Same, Anne Kilango Malecela, mmoja wa
wazungumzaji wakubwa bungeni, ambaye ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa
Wizara ya Elimu.
Alisema aliyekuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo
ya Ufundi, Jenista Mhagama amepanda kuwa Waziri wa Nchi, Sera, Uratibu
na Bunge, nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Lukuvi.
Nagu amehamia Uhusiano na Uratibu (Uwekezaji na Uwezeshaji) na Dk Harrison Mwakyembe anayehamia Afrika Mashariki (Uchukuzi).
Wengine ni mwanasiasa mkongwe, Steven Wasira
aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Kilimo akitokea Ofisi ya Rais, Uhusiano na
Uratibu, wakati Samuel Sitta anakwenda Uchukuzi akitokea Wizara ya
Afrika Mashariki

إرسال تعليق