IPTL,Tanesco sasa wagongana angani

Dar es Salaam. Wakati Kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Ltd (IPTL) chini ya uongozi wa Kampuni ya Pan African Power Solutions (T) Ltd (PAP), ikitangaza kupunguza bei ya umeme kwa asilimia 20 baada ya kufanya marekebisho makubwa ya injini za mtambo wake, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limesema halina taarifa yoyote.
“Tunatarajia hatua za upanuzi kwenda haraka kuhakikisha kuwa IPTL inatoa huduma bora ya uhakika na nafuu kwa Taifa hili. Ningependa kutoa shukrani zangu kwa uongozi wa Tanesco kwa kukubali umeme unaozalishwa na IPTL,” ilisema taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti Mtendaji wa IPTL, Harbinder Singh Sethi.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Felchesmi Mramba aliliambia gazeti hili jana kuwa hana taarifa hizo na kwamba kama kuna punguzo lolote, IPTL ilitakiwa kulijulisha rasmi.
“Taarifa hizi tunazisikia tu ila hatujaelezwa rasmi. Sisi tunachokifanya sasa ni kutekeleza maazimio yaliyotolewa na Bunge,” alisema Mramba.
Ingawa Mramba hakufafanua utekelezaji huo, katika azimio lake la saba kati ya manane, Bunge liliazimia kwamba Serikali iangalie uwezekano wa kununua mitambo ya kufua umeme ya IPTL na kuimilikisha kwa Tanesco kwa lengo la kuokoa fedha za shirika hilo.
Hata hivyo, Serikali kwa kupitia Rais Jakaya Kikwete imesema hilo likifanywa na Serikali pekee linaweza kuwatisha wawekezaji kuja nchini.
Hivi karibuni baada ya Bunge kutoa maazimio yake yaliyotokana na Ripoti ya Kamati yake ya Hesabu za Serikali (PAC), Sethi alikaririwa na gazeti hili akisema anafikiria mara mbilimbili kuendelea kuwekeza nchini.
Punguzo la IPTL
IPTL ilieleza kuwa ilifanya marekebisho ya mitambo hiyo kwa saa 36,000 kazi ambayo ilikamilika mwaka jana, huku ikitangaza pia kuwa bei yake ya umeme inatarajiwa kushuka zaidi kulingana na kushuka kwa bei ya mafuta mazito.
IPTL pia ilisema marekebisho hayo yaliyotumia zaidi ya Dola za Marekani 25 milioni, yameiwezesha mitambo yake kuwa katika nafasi nzuri ya kuzalisha umeme wa uhakika kwa kufikia megawati 100 na kuingiza kwenye Gridi ya Taifa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Sethi, kampuni hiyo imepunguza bei ya umeme wake inaoitoza Tanesco na sasa utakuwa chini ya bei ya awali iliyokokotolewa ya senti 23 Dola za Marekani kwa kilowati ikiwa na maana kwamba bei hiyo imepungua kwa senti 4.6 za Dola.

Post a Comment

أحدث أقدم