Mufti: Mataifa ya Magharibi yanatugombanisha

Tanga. Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa Shaaban Bin Simba amewataka Watanzania kutoichezea amani iliyopo na kusema wengi hawaioni thamani yake kwa kuwa wamezaliwa na kuikuta.
Aidha, amewataka wasikubali kufarakana kama baadhi ya mataifa ya Magharibi yanavyotaka kwa kubuni mbinu za kuwagombanisha ili yafanye biashara ya silaha.
Akihutubia kwenye mkesha wa Maulid ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (S.A.W) yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mazoezi, Korogwe, Mufti aliwaasa Waislamu kumuenzi kiongozi huyo kwa kuimarisha mshikamano na amani.
Alisema Mtume Mohammad (S.A.W) alipozaliwa alikuta dunia ikiwa imevurugika kwa kukosa amani na hakukuwa na utaratibu maalumu, lakini alitumia juhudi kubwa kuleta amani kwa kujenga ustaarabu kwa kuyakutanisha makundi yaliyokuwa yakigombana na kuyasuluhisha.
“Mtume Mohammad (S.A.W) alisawazisha sera za watu ambao kazi yao kubwa ilikuwa kuwagombanisha wanadamu, pia aliwakutanisha mahasimu ndipo amani ikapatikana,” alisema Mufti Simba.
Alisema njia pekee ya kudumisha siku ya kuzaliwa kwa Mtume Mohammad (S.A.W) ni kwa Waislamu kuepuka mbinu chafu za kufarakanishwa ili waonekane wavurugaji wa amani wakati ukweli ni kinyume chake.
Mufti Simba aliwataka waumini hao kujenga moyo wa kujitolea kifedha kwa ajili ya kueneza dini yao pia aliwataka kuchangia elimu akisema hakuna ya bure kuanzia ile ya dunia hadi ya dini.
Makamba
Akihutubia katika Maulid hayo, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba aliwataka Watanzania wasifanye majaribio kwa kumchagua rais anayetoa fedha kusaka wadhifa huo.
“Kiongozi wa namna hiyo, hataongoza kwa haki, watu wanaotoa fedha nyingi kusaka uongozi na wanaotumia makundi kamwe hawataongoza kwa haki. Tuwakatae viongozi wa namna hii,” alisema Makamba ambaye tayari ametangaza nia ya kuwania urais, huku akisisitiza kuwa Watanzania watafanya kosa la mwaka kumchagua rais ambaye atakuwa amepita kwa kutoa fedha nyingi katika kusaka wadhifa huo.
Akihutubia umati mkubwa wa waumini wa Kiislamu Makamba alisema: “Msikubali kuwachagua hawa wanaotumia fedha na mbinu nyingine za kuwagawa kwa makundi, kwani hao si viongozi wanaohitajika kuliongoza Taifa la Tanzania,” aliongeza: “Tanzania inahitaji kiongozi atakayewaunganisha wananchi wote kuwa kitu kimoja, mwenye busara na subira lakini si anayeutaka uongozi kwa njia yoyote hata kama ni kuwagawa kwa makundi au kutumia fedha ili mradi aweze kuchaguliwa.

Post a Comment

أحدث أقدم