Ngono, bangi ‘nje nje’ mgodini Ihanzutwa

Iringa. Wengi huisikia dhahabu, sifa zake na thamani yake. wenye fedha zao hununua vidani vya madini hayo adimu ulimwenguni na kujirembesha, lakini wale maskini kujikuta wakivaa vidani yaliyotiwa tu nakshi ya madini hayo, huku asilimia kubwa vikiwa vimetengenzwa kwa bati.
 Mbali ya wenye fedha kidogo, wapo baadhi ambao maisha yao yote hutegemea ‘kupiga roba’ watu waliovaa vidani hivyo ili kujinakshi wao pia, lakini wengi hufanya uhalifu huu kwa lengo la kuviuza na kujipatia fedha kwa njia hii isiyo halali.
 Mlolongo wa matukio yote hayo unatokana na kasi ya ongezeko la thamani ya dhahabu nchini na ulimwenguni kwa ujumla katika miaka karibuni. Mahitaji makubwa ya madini ya dhahabu yameongeza msukumo katika uzalishaji wa dhahabu kwa ujumla wake.
 Uzalishaji wa dhahabu hufanywa katika migodi mikubwa inayomilikiwa na kampuni kubwa za kimataifa, pia migodi midogomidogo inayoendeshwa na wachimbaji wadogo pia hutoa mchango mkubwa na madini wanayoyachimba ndiyo ambayo hutumiwa sana na masonara wa ndani kuzalishia vidani kama pete, hereni, bangili na vinginevyo.
 Kinachotafutwa katika machimbo madogo huwa na thamani kubwa ya kifedha na wapo waliotajirika na kubadilika kimaisha kutokana na mafanikio walioyapata katika uchimbaji wao. Hata hivyo, maisha katika migodi mingi ya wachimbaji wadogo siyo ya kawaida.
 Hali ya maisha katika maeneo haya siyo kama inavyofikiriwa kwani haiakisi uhalisia wa thamani ya madini. Mgodi wa machimbo ya dhahabu wa Ihanzutwa ni mfano halisi wa aina ya maisha waishiyo wachimbaji wadogo katika maeneo mengine nchini.
 Kama yalivyo machimbo mengine ya dhahabu hapa nchini ni dhahiri kwamba Ihanzutwa nayo inachangia uchumi wa nchi, upatikanaji wa ajira na biashara ya dhahabu. Hata hivyo, matukio ya uhalifu katika eneo la mgodi huu yanatishia maisha ya watu na mali zao. Kwa ujumla mazingira siyo salama.
 Mgodi huu uliopo kilometa zipatazo 65 kutoka Mji wa Mafinga katika wilaya ya Mufindi mkoani Iringa umegubikwa na matukio ya wizi, ngono zembe, biashara ya bangi na dawa za kulevya aina ya heroine na cocain. Biashara ya dawa za kulevya inafanywa wazi wazi pasina kificho na wahusika hawaogopi kwani hakuna usimamizi wa sheria.
Ngono yaitwa ‘show time’
Wachimbaji wengi hutumia fedha zao katika kununua ngono kutoka kwa wanawake waliojaa katika machimbo hayo. Wanawake wengi, wakiwamo mabinti wadogo wenye wastani wa umri wa miaka 17 na 18 wamejazana eneo hilo kutafuta soko la wachimbaji hao ambao kiasi kidogo cha malipo kwa huduma ni Sh10,000.
 Asilimia kubwa ya wanawake hao wanafanya kazi katika vilabu vya pombe na kuendesha biashara ya ngono kwa saa maarufu kama ‘show time’ na kurudi kuendelea kuuza pombe. Wapo pia baadhi wanaojitegemea bila ya kufanya kazi katika kilabu chochote cha pombe
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post