Kamati za Bunge zaanza kazi rasmi

Dar es Salaam. Kamati za Kudumu za Bunge zinatarajiwa kuanza kukutana na kutekeleza majukumu ya kibunge jijini Dar es Salaam kuanzia Jumanne ijayo, huku ratiba zake zikionyesha kuwa mambo yenye mvutano mkali kwa sasa yatajadiliwa.
Pia, kabla ya kuanza kwa vikao hivyo unatarajiwa kufanyika uchaguzi wa wenyeviti wapya wa Kamati za Bajeti, Katiba, Sheria na Utawala na Nishati na Madini baada ya waliokuwepo kutajwa kuhusika katika sakata la ufisadi katika Akaunti ya Tegeta Escrow na Bunge kuazimia waondolewe katika nafasi zao.
Waliotajwa katika maazimio ya Bunge, kutakiwa kuachia nafasi zao za uwenyekiti ni Andrew Chenge (Bajeti), William Ngeleja (Katiba) na Victor Mwabalaswa (Nishati na Madini).
Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Januari 14 itajadili hesabu za kampuni ya magazeti ya serikali, Shirika la Utangazaji (TBC) na Januari 15 itajadili hesabu za taarifa ya Ukaguzi Maalumu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ambayo inalalamikiwa kwa muda mrefu.
Januari 15 kamati hiyo itajadili hesabu za Bodi ya Sukari nchini, Bodi ya Korosho Tanzania na Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rujifi (Rubada).
Pia Januari 19, itajadili hesabu za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambayo watumishi wake saba walisimamishwa kazi kutokana na sakata la escrow na Januari 20 itajadili taarifa ya Kamati ndogo ya Hesabu za Serikali kuhusiana na ukusanyaji mdogo wa kodi za ardhi unaoikabili Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Pia, itajadili hesabu za Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) ambalo hivi karibuni liliingia katika mgogoro mkali na kamati hiyo na kusababisha watendaji wake kukamatwa na polisi kutokana na kuinyima kamati hiyo mikataba 26 ya gesi. Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Januari 13 itafanya ukaguzi wa miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam. Ukaguzi huo unafanyika wakati tayari kamati hiyo ikiwa imefanya ziara katika Manispaa za jiji hilo na kubaini ufisadi mkubwa. Ilala na Kinondoni zimetajwa kwenye ufisadi huo.
Baada ya ziara hiyo, Januari 14, LAAC itakutana na kujadiliana na mameya wa manispaa tatu za jiji hilo kuhusu hali halisi ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali na nidhamu ya matumizi ya fedha za umma katika maeneo yao.
Pia, itajadili taarifa ya hesabu zilizokaguliwa za Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na Karatu, Geita na Rorya
Kuanzia Januari 19 hadi 21, kamati hiyo itajadili taarifa ya hesabu za manispaa za Bukoba, Kasulu na Kwimba.
Kamati ya Bajeti itajadili taarifa za ugawaji wa fedha na utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo ya maji, barabara, uchukuzi na Tamisemi. Kamati hiyo pia itakutana na washirika wa maendeleo wa Mfuko Mkuu wa Bajeti (GBS).
Kamati na Nishati na Madini yenyewe itajadili hali ya migodi ya urani iliyopo Namtumbo na Makaa ya Mawe Mchuchuma, Liganga na Ngaka, kujadili uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini na hali ya kifedha ya Shirika la Ugavi wa Umeme (Tanesco).

Post a Comment

Previous Post Next Post