Wanaume wanahatarisha maisha yao kiafya

Wasomaji wa Piramidi ya afya, mwaka mpya na mambo mapya. Baada ya kuongelea mambo mengi yanayomhusu mama na mtoto kwa takriban miaka miwili, sasa tunamgeukia baba (mwanaume).

Kama ilivyozoeleka katika jamii zetu za Kiafrika, baba ndiye nguzo ya familia ingawa katika huduma za afya zinamweka mama na mtoto katika makundi maalumu katika kupata huduma za afya.

Kupitia kona hii nitawaletea mfululizo wa makala zinazotoa ufahamu kuhusu matatizo mbalimbali ya kiafya kwa wanaume.

Wanaume wanahitajika kuwa na tahadhari kuhusiana na afya zao, kwani unapowalinganisha na wanawake na watoto, wao wako katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali.

Jambo ambalo hata halihitaji utafiti wa kisomi, jaribu kupita katika maeneo ya burudani utagundua robo tatu ya wateja ni wanaume.

Wanaume ndiyo “wanaopiga maji” na kuvuta sigara kwa wingi na ndiyo wanaokuwa na uchaguzi wa tabia hatarishi za kupata matatizo ya kiafya.

Tabia hatarishi ni kama vile kuwa na wapenzi wengi na upande mwingine ndiyo wanaowindwa zaidi na madada wanaofanya ukahaba.

Kutokana na uwezo wao wa kufanya kazi na kujiingizia kipato kikubwa, wanaume wana uwezo wa kufanya chochote kwa kufanya ushawishi wa anasa mbalimbali.

Uwezo walio nao huweza kuwafanya wale vyakula kiholela bila kuzingatia kanuni za afya, ulevi kupindukia, hivyo kuwa na uzito mkubwa uliokithiri au kunenepa sana.

Maumbile ya kiume na mfumo mzima wa homoni zake, unamfanya mwanaume kuwa na mrundikano zaidi wa mafuta ndani ya mwili katika viungo kama moyo, ini na figo. Hii ni tofauti na mwanamke.

Hii ni moja ya sababu za wanaume wengi kuwa na magonjwa ya moyo, mishipa ya damu, kisukari, maradhi sugu ya figo,  kiharusi, magonjwa ya akili na unene ulipitiliza.

Wanaume pia huwa na maradhi ambayo huwapata wao pekee. Magonjwa hayo ni kama vile saratani ya tezi dume na kiasi kidogo cha homoni ya kiume iitwayo kitabibu ‘testosterone’.

Post a Comment

Previous Post Next Post