Siku moja baada ya Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta,
kutangaza kumsimamisha kazi kwa muda usiojulikana Kaimu Mkurugenzi wa
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), Madeni Kipande, Mkurugenzi huyo
ameibuka na kueleza kuwa ameshangazwa na uamuzi huo kwa kuwa hakuwahi
kuitwa kabla na Bodi ya Wakurugenzi wa TPA kuelezwa tuhuma hizo kama
taratibu na sheria zinavyoelekeza.
Sitta alisema alimsimamisha kazi Kipande kutokana na tuhuma za
kukiuka taratibu za zabuni pamoja na mahusiano mabaya na wateja wa
mamlaka hiyo.
Akizungumza na NIPASHE jana jijini Dar es Salaam, Kipande alisema
tuhuma zilizotolewa kwake siyo za kweli na wala hakuna taratibu zozote
za zabuni zilizokiukwa kama ilivyoelezwa na Sitta.
“Sijaitwa na Bodi kuulizwa kabla kuhusu tuhuma zilizoelekezwa
kwangu isipokuwa Waziri alikuja jana (juzi) na kusema anataka kikao cha
Bodi kuzungumza na wajumbe,” alisema.
Kwa mujibu wa taratibu, Mkurugenzi wa TPA ndiye Katibu wa Bodi,
hivyo vikao vyote vya Bodi vinapaswa kuitishwa na yeye kujadili mambo
yote yanayohusu TPA.
Kipande alisema kwa kuwa Waziri Sitta ameunda kamati kuchunguza
tuhuma zilizoelekezwa kwake, ana imani kuwa kamati hiyo itatenda haki
ili ukweli wa mambo aliyotuhumiwa ujulikane.
“Tumekutana katika kikao cha dharura cha Bodi ya Bandari kutokana
na kuzingatia malalamiko ya sehemu mbalimbali kwamba taratibu za zabuni
TPA hazikukaa sawa, zinaendeshwa katika namna ambayo hazileti imani,
nampongeza Dk. Harrison Mwakyembe, alianza vizuri kushughulikia suala
hili, lakini bado tatizo halijaisha,” alisema Sitta.
“Nimemsimamisha kazi kwa muda Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya
Bandari, Madeni Kipande kuanzia Februari 16, mwaka 2015, ili kupisha
uchunguzi unaohusu tuhuma mbalimbali zinazomkabili,” alisema na
kuongeza:
“Tuhuma hizo ni pamoja na manung’uniko kuhusiana na ukiukwaji wa taratibu za manunuzi.”
Alisema TPA ni kituo muhimu cha uchumi wa nchi kwa sababu karibu
asilimia 87 ya mapato yanatoka hapo, hivyo kunahitajika watu kufanya
kazi kwa umakini na uadilifu zaidi.
Sitta alisema hapakuwapo na uwazi katika zabuni kiasi kwamba hata
baada ya Bodi ya Zabuni kufanya maamuzi, kumekuwa na ucheleweshaji wa
kutoa barua ya kuidhinisha zabuni hizo, hivyo kuleta taswira mbaya kwa
serikali.
“Kwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Madeni Kipande, ndiye msimamizi
mkuu wa masuala yote ya bandari kuanzia leo, namsimamisha kazi hadi hapo
tume niliyoiunda kuchunguza masuala hayo itakapokamilisha kazi,”
alisema.
Sitta alitangaza kamati aliyoiunda kuchunguza suala hilo kuwa ni
Jaji mstaafu Agusta Bubeshi, ambaye atakuwa Mwenyekiti na Katibu wake ni
mfanyakazi wa Wizara ya Uchukuzi, Deogratius Kasinda.
Wajumbe wengine ni Dk. Ramadhani Mlingwa, ambaye ni Mkurugenzi
mstaafu wa Mamlaka ya Manunuzi ya Umma (PPRA); Flavian Kinundo
(Mkurugenzi mstaafu wa Masoko TPA; Hapiness Senkoro na Mhandisi Samson
Luhigo, ambao ni wafanyakazi wastaafu wa TPA.
Alisema ameamua kuwateua wastaafu katika kamati hiyo ambayo
itafanya kazi ya uchunguzi kwa wiki mbili kwa sababu watu hao hawahitaji
cheo.
Baada ya uamuzi huo, Sitta amemteua Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Awadh Massawe, kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA.
Kipande aliteuliwa Agosti, mwaka 2012 na Dk. Mwakyembe ambaye
alikuwa Waziri wa Uchukuzi, baada ya kuwasimamisha kazi vigogo sita wa
TPA akiwamo Mkurugenzi Mkuu, Ephraem Mgawe, kutokana na tuhuma
mbalimbali za wizi.
CHANZO:
NIPASHE
إرسال تعليق