Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia.
Hatua hiyo ya Nec inadaiwa kuchukuliwa kinyume cha makubaliano 
yaliyofikiwa kati yake na wadau wakuu wa uchaguzi, ambao ni vyama vya 
siasa.
Kutokana na hatua hiyo ya Nec, Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu, 
aliitisha kikao cha Kamati ya Uongozi ya Bunge jana asubuhi ili kujadili
 suala hilo kabla ya Bunge kuishauri serikali nini kifanyike.
Uamuzi huo wa Zungu ulitokana na hoja iliyotolewa na Mbunge wa 
Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia, bungeni jana, ambaye alitaka 
Bunge lisimamishe shughuli zake za jana asubuhi ili kujadili suala hilo 
aliloliita kuwa ni la ‘dharura.’
Mbatia alisema Nec juzi ilikutana na kuamua kuanza kundesha zoezi 
hilo katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Njombe bila wadau wakuu 
kushirikishwa kama walivyokubaliana kwenye meza ya mazungumzo.
Alisema makubaliano hayo yalifikiwa katika kikao cha wadau wakuu 
kilichofanyika Januari 8, mwaka huu, kupitia Kituo cha Demokrasia 
Tanzania (TCD) chini ya Mwenyekiti wake, John Cheyo, ambacho Nec 
walialikwa.
Mbatia alisema katika kikao hicho, Nec iliwahakikishia kuwa zoezi 
hilo lina changamoto kubwa na kwamba, lingeanza upya Januari 15, mwaka 
huu.
Alisema zoezi hilo lilianza mwanzoni mwa Juni, mwaka jana, lakini 
halikufanikiwa, pia likafanyika tena mwishoni mwa mwezi huo, katika 
maeneo ya mkoa wa Rukwa, vilevile likafeli. Alisema wakakubaliana kuwa 
Nec na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (Zec) wakutane na kujadili kwa 
pamoja kisha wawaelimishe wadau namna zoezi hilo litakavyofanyika kwa 
kutumia BVR ili wakubaliane kama lina maslani kwa taifa au la.
Mbatia alisema walifikia makubaliano hayo kwa kuwa iwapo jambo hilo halitaendeshwa vizuri nchi inaweza kuingia kwenye machafuko.
Hata hivyo, alisema juzi Nec ilikutana na kuanza kufanya utaratibu 
wa kuendesha zoezi hilo katika mikoa hiyo bila wadau wakuu kushirikishwa
 kama walivyokubaliana kwenye meza ya mazungumzo.
Alisema katika kikao hicho, walikubaliana kuwa zoezi hilo 
lihakikishe linafanyika kwa uadilifu, uaminifu na kwa pande zote 
kushirikishwa.
Mbatia alisema wadau waliokutana katika kikao hicho, wanatoka vyama
 vyote vya siasa, kikiwamo Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho 
kiliwakilishwa na Makamu wake Tanzania Bara, Philip Mangula.
Alivitaja vyama vingine vilivyoshiriki kikao hicho cha wadau kuwa 
ni pamoja na Chadema, iliyowakiloshwa na Katibu Mkuu wake, Dk. Willibrod
 Slaa, CUF (Prof. Ibrahim Lipumba), NCCR-Mageuzi (James Mbatia), TLP 
(katibu mkuu wake) na vyama vingine visivyokuwa na uwakilishi bungeni.
Alisema jambo hilo lina maslahi mapana kwa umma na kwamba, katika kikao hicho, Nec ilieleza mambo mengi sana.
"Tukawashauri kwa nia njema kwamba, ni bora tukae, tuzibe ufa kabla ya kujenga ukuta tuaminiane," alisema Mbatia.
Alisema pia waliisisitiza kuwa Nec ulazima wa kulifanya jambo hilo 
ili kuhakikisha kwenye uchaguzi mkuu malalamiko yanapungua na 
kuhakikisha yaliyotokea katika uchaguzi mkuu wa Kenya, Ghana, Msumbiji 
na Malawi yasitokee nchini.
Kutokana na hali hiyo, alisema kwa mujibu wa kanuni ya 47, Bunge 
linapaswa kutekeleza matakwa ya ibara ya 63 (2) ya katiba ya nchi 
inayotambua kazi ya Bunge kuwa ndiyo chombo kikuu cha kuisimamia na 
kuishauri serikali ili zoezi hilo lifanyike kwa uadilifu na kwa ufanisi 
mkubwa kuepuka mtatizo yaliyotokea katika nchi hizo yasitokee hapa 
nchini.
"Na hakuna jambo jema kama kuaminiana katika jambo lenye maslahi kwa taifa," alisema Mbatia.
Akijibu hoja hiyo, Zungu alisema anakubaliana kwamba, jambo hilo ni
 la muhimu, kukaa pamoja na Bunge kuwa ni chombo cha kuishauri serikali.
Hivyo, akaiagiza serikali kuanzia wakati huo kukaa pamoja na Mbatia wakalijadili kwenye Kamati ya Bunge ya Uongozi.
Hata hivyo, Kamati ya Uongozi, imelipeleka suala hilo kwenye Kamati
 ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala ili likafanyiwe kazi.
Katika kikao hicho, serikali imesisitiza kuwa imeshatoa fedha za kutosha kwa ajili ya BVR.
     CHANZO:
     NIPASHE
    

Post a Comment