CCM hatua moja kuelekea uchaguzi

Dodoma. Wakati Rais Jakaya Kikwete akitarajiwa kutua mjini hapa mwishoni mwa wiki hii kuendesha kikao cha Baraza la Mawaziri, huku Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), ikitarajiwa kukutana muda wowote kuanzia wiki ijayo kujadili pamoja na mambo mengine, mchakato wa Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu.
Chanzo chetu cha habari kilisema jana kuwa Kikwete atakuwa mjini hapa wikiendi hii kuendesha kikao cha Baraza la Mawaziri.
Hata hivyo CCM imeanza hatua ya kwanza kuelekea Uchaguzi Mkuu wakati kikao cha NEC kikitarajiwa kufanyika mwezi huu kupanga tarehe na utaratibu mzima wa uchukuaji na urejeshaji fomu kwa wagombea wa chama katika ngazi za urais, ubunge na udiwani.
Tayari Rais Kikwete amepuliza kipenga cha mbio za urais kwa CCM katika sherehe za miaka 38 ya kuzaliwa kwake wakati wa maadhimisho yaliyofanyika mkoani Ruvuma, akiwataka wenye sifa wajitokeze kuchukua fomu huku akisema: “Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba, mwaka huu wa kupata rais wa awamu ya tano, utakuwa wa kihistoria.”
Waliotangaza, wanaotajwa
Hadi sasa makada wa CCM waliotangaza nia kuwania urais ni Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Mawasiliano, January Makamba; Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla; Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu.
Pia wapo wanaotajwa kwamba huenda wakajitokeza mchakato huo utakapoanza rasmi ambao ni Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba; Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi; Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta na mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye.
Wengine ni Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Asha - Rose Migiro; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira.
Kura ya Maoni
Katika kikao cha NEC ambacho kitakutana muda wowote wiki ijayo inadaiwa kuwa suala la kura ya Maoni huenda likaibua mjadala mkubwa kutokana na kuibua mijadala mingi hasa kutokana na kile kilichoelezwa kuwa muda wa utekelezwaji wake hautoshi.
Viongozi wa vyama vya upinzani wameshatangaza kuwa hawatashiriki katika mchakato huo.
Jana, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi na Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia aliwasilisha bungeni hoja za kutaka kuahirishwa kwa mchakato huo akisema uko nyuma ya wakati.
- Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم