KAKA ADAIWA KUMTOROSHA DADA YAKE KWA MUME

ALLY Issa anayeishi Mombasa nchini Kenya, anadaiwa kumtorosha dada yake Hasina Issa (22)  aliyekuwa akiishi na mumewe, Baraka Ally (32), Mbezi Mwisho jijini Dar es Salaam.Tukio hilo lilitokea siku ya mkesha wa Siku ya Wapendanao ‘Valentine’s Day’.
Hasina Issa siku ya harusi yake.
Akizungumza na gazeti hili mwishoni mwa wiki iliyopita, Ally alisema alitoa taarifa polisi na kufunguliwa jalada namba KMR/RB/1996/15 Kimara, akiamini mke wake ametoroshwa.
Alisema mkewe huyo, aliyemuoa Julai 6, mwaka 2013 Tandale, alitoweka baada ya kaka yake huyo akiwa na mkewe Mzungu, kuwatembelea nyumbani kwao.
“Ninakumbuka siku mbili kabla ya kutoroshwa, nikiwa kazini, shemeji yangu mmoja alinipigia simu akiniambia nikamuone shemeji yangu mwingine wa Mombasa ambaye alikuwa amekuja na mwanamke wa Kizungu.
“Nilipotoka kazini nilikwenda Tandale ambako nilimkuta akiwa na huyo Mzungu, alisema ametutembelea hivyo niwapeleke kwangu, wana hamu ya kumuona mke wangu.“Walikodisha teksi hadi nyumbani, tulifika saa mbili usiku, wakasema kisipikwe chakula bali tukale hotelini, tulifurahi sana, wakawa wanatupiga picha, baadaye wao walienda hotelini Sinza walikofikia wakiahidi kurejea kesho yake.
“Lakini nikapata safari ya kikazi kwenda Mtwara kwa siku moja, niliporudi mke wangu alinikaribisha vizuri, asubuhi nikaenda kazini, nikiwa njiani alinipigia simu mara nne kwa nyakati tofauti akiniuliza nilipokuwa, haikuwa kawaida yake kufanya hivyo.
“Muda si mrefu nami  nikawa nampigia hadi mara tano lakini hakupokea, nilipotuma ujumbe hakujibu, nilipofika nyumbani sikumkuta,” alisema Ally.Aliongeza kuwa alipojaribu kumpigia shemeji yake kumuulizia alipokuwa dada yake, alimjibu kuwa hajui kwani kwa wakati huo alikuwa mjini Bukoba akiwa njiani kuelekea Uganda.
Alisema alipowasiliana na wakwe zake Tandale, Dar alitakiwa kwenda huko, lakini cha kushangaza alipofika, alitakiwa kuandika talaka ya kumtaliki mkewe.
“Nikawauliza nitatoaje talaka wakati mke wangu hayupo? Sasa nitampa nani? Simu zao hazipatikani, ila mmoja wa shemeji zangu anayenipenda aliniambia mke wangu alionekana na kaka yake wa Mombasa kituo cha mabasi Ubungo, ndipo nikaenda kutoa taarifa polisi.”

Post a Comment

Previous Post Next Post