Matokeo haya kidato cha nne yanatufunza nini?

Jumamosi iliyopita, Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), lilitangaza matokeo ya mtihani wa kidato cha nne wa mwaka 2014.
Wanafunzi waliomaliza kidato cha nne mwaka 2014 ndiyo waliohitimu darasa la saba mwaka 2010. Mwaka huo waliofaulu walikuwa 478,912 sawa na asilimia 53.51 ya wanafunzi 895,013 waliofanya mtihani.
Safari yao ya kimasomo imekuwa ikiendelea huku wakiwaacha wenzao njiani, kwani Serikali ikatangaza kuwa wanafunzi 456,350 ndiyo waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2011, ikiwa ni sawa na asilimia 95.3 ya wale waliofaulu mtihani wa darasa la saba.
Hii inamaanisha kuwa waliwaacha wenzao 22,562 ambao hawakuweza kuchaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2011. Wengine wameishia njiani kwani ni wanafunzi 288,365pekee ndio waliofanya mitihani ya kidato cha nne. Wanafunzi 167,985 kati ya 456,350 waliofaulu kujiunga kidato cha kwanza 2011 walipotelea njiani mpaka sasa. Hii ni idadi kubwa .
Wakati waziri Kawambwa anasoma matokeo yao ya darasa la saba mwaka 2010, alisema walifaulu Kiingereza kwa asilimia 36.47 na Hisabati kwa asilimia 24.70. Hii ndiyo sababu wanafunzi hawa hawakufaulu mtihani wa hesabu kidato cha nne kwakuwa hawakuwa na msingi bora tangu wakiwa shule ya msingi.
Ufaulu wa Hesabu umeshuka hadi asilimia 19.58 tofauti na 24.70 walizopata kwa mtihani wa darasa la saba mwaka 2010. Hata hivyo, inaonekana ufundishaji wa Kiingereza wakiwa sekondari uliimarika kidogo hadi kupata ufaulu wa asilimia 55.10 katika kidato cha nne kutoka asilimia 36.47 za ufaulu wa darasa la saba mwaka 2010.
Mwaka 2014 kulikuwa na vituo vya mitihani 5419 kukiwa na nyongeza ya vituo 1064 ukilinganisha na vituo 4355 vya mwaka 2013. Miaka ya hivi karibuni, baraza limekuwa likitenganisha makundi ya vituo kwa kigezo cha idadi ya watahiniwa.
Lipo kundi la watahiniwa wasiozidi 40 lenye vituo 2,097 na lile la watahiniwa zaidi ya 40 lenye vituo 2,322. Hii inamaanisha kuwa shule za sekondari zimeongezeka zaidi nchini.
Matokeo ya kidato cha nne
Mfumo wa sasa wa ufaulu unatokana na asilimia 30 za maendeleo ya shule na asilimia 70 za mtihani wa mwisho. Hivyo mfumo huu unaonyesha kuwa umechangia kwa kiasi kikubwa aina ya matokeo yaliyotangazwa ya wahitimu wa mwaka 2014. Hebu tuchimbue zaidi tuone kilichopatikana na tufanye tathmini zaidi.
Mwaka 2013, ufaulu ulikuwa kwa asilimia 58.25 yaani wanafunzi 235,227 walifaulu. Kiwango hiki kilijumuisha hata wale waliopata daraja la nne. Lakini wale waliopata daraja la kwanza hadi la tatu walikuwa 74,324 tu, ambao ni sawa na asilimia 21.09. Waliopata daraja la nne walikuwa 126,828 na wahitimu 151,187 walipata daraja sifuri.
Mwaka 2014 wametumia mfumo mpya wa kupanga madaraja kwa njia ya wastani wa ufaulu (GPA). Waliofaulu daraja la kwanza hadi la tatu kwa mfumo huu mpya ni 73,832 sawa na asilimia 30.72. Kati ya hawa, wasichana ni 27,991 na wavulana ni 45,841.

Post a Comment

أحدث أقدم