Mtifuano mkubwa majimbo ya Kigoma Kaskazini, Kusini, Muhambwe na Buyungu

KIGOMA KASKAZINI
Tuliangalie jimbo hili tangu mwanzo wa mfumo wa vyama vingi. Mwaka 1995 wananchi wa Kigoma Kaskazini waliamini watachagua upinzani, hasa NCCR –Mageuzi. Kwa bahati mbaya matokeo yalipotangazwa, mgombea wa CCM alishinda kwa kura kidogo, huku kura zake zikizidiwa mbali na mchanganyiko wa kura za mgombea wa NCCR-Mageuzi na vyama vingine vya upinzani.
Mwaka 2000 mgombea wa CCM Halimenshi Mayonga alishinda huku vyama vya upinzani vikigawana kura na kusalimu amri kwa CCM kwa mtindo uleule wa 1995. Mara baada ya uchaguzi wa 2000 wakati, ambapo Chadema ilikuwa ikinoa makada wenye uwezo mkubwa akiwamo Zitto Kabwe, mapinduzi ya kifikra yalizidi kukua katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, huku Zitto akiendelea kujipanga wakati akimalizia masomo yake Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Mwaka 2005 ulikuwa ni mwaka muhimu kwa siasa za Mkoa wa Kigoma. Huu ni wakati ambapo Jimbo la Kigoma Kaskazini lilimpeleka bungeni kijana wa miaka 29, huyu ni Zitto Kabwe. Zitto alipata ushindi wa asilimia 51.1 uliotokana na kura 28,198 dhidi ya mgombea wa CCM na mbunge aliyekuwa akimaliza muda wake Mayonga Halimenshi aliyepata asilimia 39.6 zilizotokana na kura 21,822.
Wagombea wa CUF na NCCR-Mageuzi kwa pamoja walipata asilimia 8.8 ya kura zote, kutokana na kura 4,824. Mwaka huo, mwanya wa wapinzani kugawana kura na kuiachia CCM ushindi haukufua dafu mbele ya mikakati kabambe ya Zitto na chama chake. Zitto alikuwa ‘Rafiki wa Mbowe’ hasa na alikuwa tegemeo muhimu la Chadema.
Kipindi cha 2005–2010 kilishuhudia harakati nyingi kwa nchi nzima kwa jumla. Pia, mmoja wa wanasiasa waliong’ara na kufanya vyama vya upinzani vizidi kukubalika huku vijana wakianza kujitanabaisha kama tumaini la pekee katika nchi yetu, ni Zitto Kabwe. Zitto wakati huo akishirikiana na Dk Wilbrod Slaa wakifanya kazi chini ya Hamad Rashid wa CUF (Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni) walifanya kazi kubwa bungeni na nje ya Bunge. Wakati ule ungeweza kudhani kuwa wao ndiyo walikuwa viongozi wa kambi ya upinzani bungeni.
Harakati za Zitto na wenzake katika wakati huo naweza kusema zilikuwa chanzo cha Chadema kuaminiwa na kukua katika majukwaa ya wananchi wa kawaida, huku vijana wengi wakijiunga na siasa kwa kuona uthubutu mkubwa alioufanya Zitto Kabwe na wenzake.
Mwaka 2010 Zitto aligombea tena, mara hii CCM ikimleta Robinson Fulgence Lembo na CUF ikimsimamisha mgombea mwenye nguvu, Omary Mussa Nkwarulo. Matokeo yalipotangazwa Zitto Kabwe aliwashinda wapinzani wake kwa kupata kura 23,366 (asilimia 48.57), dhidi ya kura 18,352 (asilimia 38.15) za Fulgence wa CCM, huku Nkwarulo wa CUF akipata kura 4,839 (asilimia 10.06). Ukitizama utaona kuwa ushindi wa Zitto haukuporomoka sana, ulishuka kwa asilimia tatu tu ukilinganisha na ule wa mwaka 2005.
Zitto amefanikiwa kuliongoza Jimbo la Kigoma Kaskazini kwa kipindi cha pili 2010–2015 na ametangaza kutogombea tena mwaka huu na badala yake anakwenda Kigoma Mjini ambako Peter Serukamba wa CCM naye ametangaza kuondoka na kuja kugombea Jimbo la Kigoma Kaskazini.
Jambo moja ambalo naliona hapa Kigoma Kaskazini ni kuwa, Zitto akishaondoka itavipasa vyama vya Ukawa vitafute mgombea imara ambaye anaweza kutoa ushindani mkubwa kwa Peter Serukamba ama mbunge mwingine yoyote wa CCM. Chama cha ACT Tanzania nacho kinakuja kwa kasi kubwa katika Jimbo la Kigoma Kaskazini na kuna wananchi wana hasira za uhusiano mbaya kati ya Zitto na chama chake, Chadema.
Ukichanganya mambo yote hayo unaweza kuanza kuona kila dalili ya upinzani kufanyiana vurumai na mwishowe jimbo kuangukia mikononi mwa CCM. Kwa siasa za Kigoma jambo hilo linawezekana sana. Hatma ya kisiasa ya Zitto itategemeana sana na karata atakazocheza ikiwa atagombea Kigoma Mjini kama inavyosemwa.
Ikiwa kweli anakwenda Kigoma Mjini itabidi ajikaze kisawasawa. Pamoja na kuungwa mkono katika maeneo kadhaa hapo Kigoma Mjini, huwezi kudharau nguvu ya vyama vya Ukawa ikiwa vitaweka mgombea mmoja kwani Zitto hawezi kugombea tena kupitia Chadema na labda atatumia Chama cha ACT Tanzania ambacho kimefanya harakati zake nyingi mkoani Kigoma na hata kupata matokeo muhimu katika baadhi ya maeneo kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa
- Zaidi Soma Hapa(Mwananchi)

Post a Comment

Previous Post Next Post