Mvua zajeruhi watu 12, kubomoa nyumba 128 Kibaha, Bagamoyo.

Makamu wa Rais, Dk Gharib Bilal.
Mkoa wa Pwani umekumbwa na maafa kufuatia mvua kubwa zilizoyesha mapema wiki hii zikiambatana na kimbunga na radi katika wilaya za Kibaha na Bagamoyo, kujeruhi watu 12, kubomoa nyumba 128 na nyingine kuezuliwa paa.
 
 Hayo yalisemwa katikati ya wiki hii na Mkuu wa Mkoa wa Pwani,  Evarist Ndikilo wakati akitoa salamu za mkoa wake kwa Makamu wa Rais, Dk. Gharib Bilal wakati wa hafla ya uzinduzi wa barabara ya Msoga- Msolwa yenye urefu wa kilomita 10 na ukaguzi wa mzani wa Vigwaza.
 
Ndikilo alisema mvua hizo zilizonyesha kwa saa mbili mfululizo katika wilaya hizo, zimesababisha  zaidi ya watu 200 kukosa mahali pa kuishi, wengi wao wakiwa ni wa Jimbo la Chalinze lililopo wilayani Bagamoyo.
 
Alisema tathimini ya awali inaonyesha katika kijiji cha Msoga,  nyumba 47, Shule ya Msingi Msoga na Ofisi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya kata zimeathiriwa na mvua hizo na watu  11 kujeruhiwa.
 
Alisema vilevile katika kijiji cha Tonga nyumba nne zimeathirika, kijiji cha Ngeta Kibaha Vijijini nyumba 77 na mtu mmoja kujeruhiwa.
 
 Alisema majeruhi hao, walipelekwa katika zahanati ya Msoga na kituo cha afya Chalinze kwa matibabu huku baadhi yao wakiruhusiwa.
 
Alisema majeruhi  wawili baba na mtoto wake wamelazwa Hospitali ya Tumbi  Kibaha kwa uangalizi  zaidi wa madaktari.
 
 Alisema  Serikali ya Wilaya ya Bagamoyo na Kibaha kwa ushirikiano na Serikali ya Mkoa zinaendelea kufanya tathimini ya maafa hayo ili kuwasaidia waathirika ambao kwa sasa wanahifadhiwa kwa ndugu, jamaa na jirani zao.
 
Kufuatia maafa hayo, Dk. Bilal alitoa pole kwa wakazi wa Kibaha na Bagamoyo na kuahidi kuwa Ofisi yake itachangia Sh.  5,000,000 kuwasaidia.
 
 Waziri wa Ujenzi , Dk. John Magufuli naye aliahidi kuwachangia Sh. milioni 1 na Mbunge wa  Chalinze Ridhiwan Kikwete kiasi kama hicho.

Post a Comment

Previous Post Next Post