Ajenda 10 za mrithi wa JK

Dar es Salaam. Wakati mjadala wa majina ya watu wanaotaka kuwania urais umepamba moto, baadhi ya wasomi, wachambuzi na wasomaji wa gazeti hili wamesema badala ya kukimbilia majina, wagombea hao wanatakiwa kueleza jinsi gani watakavyokabiliana na ajenda 10 muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
Ajenda hizo kwa mujibu wa wadau wa kada mbalimbali walioongea na Mwananchi kuhusu vipaumbele vya taifa kwa sasa, ni tatizo la ajira, changamoto za kuinua kilimo, kutoa elimu bora, kusimamia makusanyo ya kodi, rasilimali za taifa na kuboresha miundombinu ya usafiri.
Wagombea hao pia watatakiwa kueleza jinsi watakavyoondoa migogoro ya wakulima na wafugaji, matumizi sahihi ya ardhi, mapambano dhidi ya rushwa, uhalifu na matumizi ya dawa za kulevya, kwa mujibu wa marejeo ya habari mbalimbali yaliyofanywa na gazeti la Mwananchi.
Kwa kawaida, vyama vya siasa huandaa ilani zake za uchaguzi ambazo ndiyo mwongozo wa kampeni za kutafuta kura kwa wananchi kwa ajili ya wagombea wake wa urais, ubunge na udiwani, lakini watatakiwa kuzingatia hoja hizo muhimu.
Katika mahojiano na wadau mbalimbali, gazeti la Mwananchi lilitaka kujua ni mambo gani ambayo wananchi “wanataka yawe ajenda kuu kwenye kampeni za uchaguzi ili kuikwamua nchi” kutoka hapa ilipo, na majibu yao yalionyesha suala la ajira, kilimo, afya, rasilimali za taifa, usafiri, maji, rushwa na migogoro ya ardhi kuwa ndiyo mambo ambayo hayajafanyiwa kazi na hivyo wanataka kusikia wagombea watakavyokabiliana nayo.
“Kwanza tunahitaji utawala bora unaosimamia haki, Serikali inayofanya uamuzi sahihi,” alisema mwanasheria wa jijini Dar es Salaam, Felix Kibodya kabla ya kutaja mambo ambayo anaona yanafaa kupewa kipaumbele.
Usimamizi wa rasilimali
Kibodya, ambaye amewahi kuwa rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), alisema rasilimali zikisimamiwa na kutumika vizuri, zitalinufaisha Taifa kwa kiasi kikubwa.
“Kuna viongozi katika nchi hii waliwahi kueleza wazi kwamba rasilimali zikibaki ardhini haziozi. Tukifanya mchezo rasilimali hizi zitakwisha. Suala hili linaenda sambamba na ubinafsishaji tulioufanya miaka ya nyuma, sasa ndiyo tunaaza kuona ubaya wake,” alisema.
Alikuwa akizungumzia rasilimali kama dhahabu, chuma, shaba, platinum, nickel, almasi, tanzanite, rubi, garnet, emerald, sapphire na maliasili nyingine kama gesi na mafuta.
Kati ya madini hayo, dhahabu na almasi ndiyo zimekuwa tegemeo kubwa kwa uchumi wa Tanzania, wakati kugundulika kwa gesi na uwezekano wa kupatikana kwa mafuta kumeinua matarajio ya maisha bora kwa wananchi na wakati fulani Rais Jakaya Kikwete aliwahi kunukuliwa akisema “atakuwa Rais wa mwisho kuiacha nchi maskini”.
Lakini kilio kikubwa cha wadau imekuwa ni mikataba, ambayo imeelezwa kuwa ni ya siri na hainufaishi Taifa na badala yake inanufaisha wawekezaji na wajanja wachache
- Mwananchi Bofya Hapa

Post a Comment

Previous Post Next Post