Prof Ndulu: Utalii unaongoza kulingizia taifa pato la kigeni

Dar es Salaam. Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu amesema hivi sasa sekta ya Utalii ndiyo inayoongoza kwa kuliingizia taifa mapato ya kigeni baada ya kuipita sekta ya dhahabu iliyoshuka kutokana na kuporomoka kwa bei kwenye soko la dunia.
Akizungumza leo kwenye mkutano uliojadili mabadiliko ya kiuchumi Tanzania, Profesa Ndulu amesema sekta ya utalii inaliingizia taifa dola 2bilioni, dhahabu (dola 1.7bilioni), bidhaa za viwandani (dola 1.3bilioni) na huduma za usafirishaji mizigo ni dola 800milioni.
Sekta ya utalii inaingiza Dola za Marekani 2 bilioni kwa mwaka ikifuatiwa na dhahabu inayoipatia nchi Dola za Marekani 1.7 bilioni, bidhaa za viwanda vinazouzwa katika nchi mbalimbali barani Afrika inaingiza Dola za Marekani 1.3bilioni ikifuatiwa na usafirishaji wa huduma za mizigo katika nchi jirani ambapo zinaingiza Dola za Marekani 800milioni.
Profesa Ndulu amesema ongezeko la mapato kwenye viwanda ni sawa na fedha zote za kigeni zinazotokana na mazao sita makubwa ya kilimo nchini kwa pamoja.
“Mfumo wa kuingiza mapato ya fedha za kigeni nchini umebadilika sana, mimi na imani kuwa nafasi yetu kijiografia inatupa fursa kubwa sana ya kuhudumia wengine walioko mbali na bahari,” alisema Profesa Ndulu.
Akizungumzia kuhusu nafasi ya kilimo, Profesa Ndulu almeema iwapo viwanda vingi vitajengwa karibu na wakulima, mfumo wa uchumi katika maeneo hayo utaimarika kuliko ilivyo sasa.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba, alisema jambo muhimu linalotakiwa kujadiliwa ni namna gani pato la viwanda litaongezwa zaidi kwa kuwa hivi sasa kuna changamoto ya ukosefu wa umeme wa kutosha.
“Kwa muda mrefu umeme umekuwa mdogo na ufisadi umeathiri sana sekta ya umeme kiasi kwamba Tanesco inashindwa kuzalisha umeme wa kutosha kwa bei nafuu,” amesema Profesa Lipumba.
Pia, amesema uwepo wa bandari inayotumiwa na nchi jirani haujafanikiwa kuliingizia taifa mapato ya kutosha kutokana na udhaifu ya kiuongozi.
“Uongozi wa bandari unabadilika kila wakati, kila waziri akija anatafuta mtu wake ambaye atamsaidia katika ulaji kwa hiyo anabadilisha uongozi uliopo analeta wengine matokeo yake bandari yetu haiongozwi kwa ufanisi unaohitajika,” amesema Profesa Lipumba.
Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe, amesema matokeo yaliyotolewa na BoT yanaonyesha kuwa uchumi hivi sasa unakwenda kwa watu wachache na kuondoka kwa watu wengi ambao ndio wapo kwenye sekta ya kilimo, hivyo si jambo la kulifurahia.
“Taarifa hii inaashiria kwamba watakao nufaika na uchumi ni watu wachache, wamiliki wa migodi, kampuni za kigeni zinazohusika na utalii na wafanyabiashara wachache hasa kwenye sekta ya usafirishaji na hivi sasa asilimia 99 ya mizigo yote inasafirishwa kwa malori,” amesema Zitto

Post a Comment

Previous Post Next Post