Shahidi: Mtuhumiwa alimuua Mwangosi bila kukusudia

Daud Mwangosi.
Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Dodoma, Frola Mhele, ameambia Mahakama Kuu Kanda ya Iringa kuwa aliyekuwa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU),  Pcificus Clerofas Simon, alipelekwa kwake kuungama kumuua aliyekuwa Mwandishi wa Habari wa Kituo cha Televisheni Chanel Ten Mkoa wa Iringa, Daud Mwangosi, (pichani) kwa bomu bila kukusudia.
Mhele aliyasema hayo jana mbele ya Jaji wa Mahakama hiyo, Paulo, Kihwelo, wakati akitoa ushahidi wa kesi ya mauaji ya Mwangosi.
Hakimu huyo ambaye ni shahidi wa tatu, alidai kuwa  mtuhumiwa huyo alipelekwa kwake kuungama wakati akiwa Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mjini Iringa.
Alidai Septemba 5, 2012 saa 7:24 mchana, polisi walimpeleka mtuhumiwa huyo katika mahakama hiyo kwa ajili ya ungamo na kuchukua maelezo.
Alidai mtuhumiwa huyo alimweleza kuwa amefikishwa mahakamani hapo  kwa  sababu anatuhumiwa kwa kesi ya mauaji.
Shahidi huyo alidai alimkagua mtuhumiwa mwilini mwake na kumkuta akiwa na jeraha bichi kwenye mkono wake wa kulia katika kidole cha kati kutoka mwisho na majeraha ya zamani.
Mhele alidai alipomuuliza kuwa jeraha amelipatia wapi, alimjibu alilipata wakati bomu lilipolipuka na kwamba hakujua kama amepata jeraha hilo.
Alidai mtuhumiwa huyo katika maelezo yake, alimweleza kuwa Septemba 2, 2012 ilitokea kazi kijiji  cha Nyololo Wilaya ya Mufindi ambako kulikuwa na mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambao haukua rasmi.
Alidai mkutano huo hakuwa rasmi kwa sababu wafuasi wa Chadema na viongozi wao walikaidi amri ya Polisi ya kuzuia kufanyika licha ya kutangaziwa ilani mara tatu.
Alidai mtuhumiwa huyo aliendelea kumweleza kuwa askari waliokuwapo kwenye eneo hilo waliamriwa kuwatawanya kwa kutumia mabomu ya machozi.
Alidai mtuhumiwa huyo alimweleza kuwa yeye na  askari wengine walisikia sauti ya askari akipiga yowe kuomba msaada na mlio mkubwa wa kishindo, lakini yeye hakujua mlio ule  ulitokea wapi.
“Mshitakiwa katika maelezo yake  alieleza kuwa inawezekana ni yeye alipiga bomu bila kujua,” alidai na kuongeza:
“Baada ya kutoka eneo la tukio na kufika kambini waliitwa kwenye mstari na kugundulika kuwa silaha aliyoibeba yeye ndiyo ilitumika kupiga lile bomu na kumuua Mwandishi Daudi Mwangosi, lakini yeye hakukusudia.”
Shahidi wa nne, Lewis Tiekya (29) ambaye alikuwa mtunza ghala la silaha msaidizi, alidai kuwa siku ya tukio alipokea simu kutoka kwa Mkuu wa FFU,  Said Mnunka, saa 12:30 asubuhi akimweleza kuwa anahitajika haraka katika ghala la silaha kwa sababu kuna dharura imetokea wilayani Mufindi.
Tiekya alidai alimwamuru atoe silaha ili kwenda kuweka amani kijijini hapo.
Alidai  silaha ya mtuhumiwa iliyokuwa na namba 040824 ilirudi kama ilivyo kwa sababu hakujua kama ndiyo imetumika kupiga bomu hilo.
Alidai wakati huo alitoka na  mabomu 15 ya kishindo kikubwa na 22 ya moshi ya kurusha kwa mikono,  risasi za SMG 60 ambazo hazikurudi hata moja.
Mtuhumiwa huyo anatetewa na Wakili Rwezaula Kaijage.
Mahakama hiyo ilipokea vielelezo vya kesi hiyo ambavyo ni silaha ya kishindo namba 040824, maelezo ya ungamo la mtuhumiwa na kitabu cha orodha ya majina ya askari wanaochukua na kurudisha silaha ghalani.
Wakili wa Serikali Ladislaus Komanya, alidai kuwa mashahidi wawili wameshindwa kufika kwa sababu hati ya kuitwa haikuwafikia na mmoja  ameomba udhuru kwa sababu ameuguliwa ghafla.
Komanya aliiomba mahakama kuwa ombi la pili la utuzwaji wa kielelezo cha mashitaka namba nne ambayo ni bunduki mahakama itoe ili itunzwe na Jeshi la Polisi hadi itakapohitajika kwenye kikao kijacho.
Komanya alidai kielelezo namba tano ambacho ni kitabu cha orodha ya kuchukua silaha na kurudisha irejeshwe kwa upande wa mashtaka kwa sababu inatumiwa na jeshi  hilo.
Aliomba karatasi ambayo ilitumika siku hiyo kwa ajili ya kuchukua silaha, ibaki mahakamani hapo kwa ajili ya ushahidi.
Wakili Kijage hakuweka pingamizi kuhusu kielelezo namba nne kutunzwa na polisi, kadharika na  kielelezo namba tano.
Hata hivyo, aliomba shauri lipewe kipaumbele katika kikao kijacho kwa sababu mtuhumiwa yupo rumande.
Mwangosi aliuawa Septemba 2, mwaka 2012  katika kijiji cha Nyololo, wilaya ya Mufindi wakati akiwa kwenye majukumu yake ya kazi kwenye mkutano  wa Chadema wa kufungua tawi la chama hicho.
Jaji Kihwelo aliahirisha kesi hiyo mpaka Msajili wa Mahakama atakapopanga kikao kijacho kutokana na mashahidi wengine watatu kutofika mahakamani kutoa ushahidi.

Post a Comment

أحدث أقدم