Tumeufikia mwaka wa uchaguzi. Ni mwaka wa furaha kwa wengine
kwani wameishi kwa matumaini ya kupata nafasi za uongozi kwa kipindi
wanachojua wao na hivyo mwaka huu ni mwaka wao wa kujaribu bahati yao.
Ni mwaka wa kihoro kwa wengine haswa wale
waliopita kipindi kilichopita kwa kutoa ahadi ambazo hata asilimia moja
ya ahadi hizo hazijatekelezwa, hivyo wana wasiwasi kama wapiga kura
watawapa ridhaa tena. Wanasiasa kwa wakati huu hawalali, wanahaha
kutafuta namna ya kuwafanya wapiga kura wawaamini na kuwapa kura zao.
Kuna mikakati ya mgombea mmoja mmoja na kuna
mikakati ya pamoja kwa kiasi kikubwa ikiwa chini ya vyama vyao. Kwamba
kila mtu anajitahidi kuonesha kwamba chama chake ndicho haswa
kinachotakiwa kupewa ridhaa ya wananchi.
Kelele ni nyingi sana za kipi chama bora. Na sisi
wapiga kura tumeunganishwa kwenye kelele hizo hizo hata tunajisau kwamba
kitakachotuhudumia siyo nembo ya chama bali ni watu watakaosimamishwa
na chama kile.
Tumeunganishwa katika kelele hizo kiasi kwamba
hatujali tena nani tunamchagua ili mradi tu awe ametoka katika chama
kile ambacho kelele zake zimetuvutia zaidi. Tunavutiwa na hizo kelele
kiasi kwamba hata pale wanapotutusi kwa kutuambia kwamba chama chao hata
kikisimamisha jiwe litachaguliwa tu, tunapiga makofi ya furaha kwa
kauli hiyo na kweli tunalichagua jiwe lilisimamishwa. Tumeshuhudia watu
wa ajabu ajabu wakiingia katika nafasi mbalimbali ambao mwisho wa siku
tunagundua hawana mchango wowote katika kuboresha maisha yetu.
Jamani hebu tubadilike na kuwachagua viongozi kwa
ajili yetu. Tujitathmini maamuzi tuliyoyafanye katika chaguzi za
serikali za mitaa zilizopita karibuni, tuwaangalie kama wanatosha na
kama hawatoshi tujiulize walipataje nafasi?
Kama kweli mwanasiasa alifanikiwa kukushawishi
kumchagua mtu asiye na uwezo kwa kelele za kukiunga mkono chama basi
ujue unaishi katika karne ambayo viumbe vilivyokuwepo wakati huo vyote
vimetoweka na kuwekwa katika kitabu cha historia yaani wewe hupashwi
kuishi katika ulimwengu huu wa leo.
Utashawishikaje kuchagua uozo wakati unajua fika
kwamba huyo unayemchagua unamchagua kwa ajili ya kukuondolea maumivu
yako ya; kukosa maji, kukosa zahanati, kukosa usafiri, kuzingirwa na
vibaka katika eneo lako na mengine mengi. Kwa nini maumivu hayo yasiwe
ndiyo mwongozo wako wa kusema mtu nitakayemchagua ni yule ambaye
anaelekea kwanza kuyafahamu maumivu hayo na pia anaonesha ana mbinu za
kupunguza kama siyo kuondoa maumivu hayo? Na tufunguke na kusema
hatutarudia makosa tuliyoyafanya katika chaguzi zilizopita.
Tujikumbushe ulaghai tuliopewa wakati wa chaguzi
za serikali za mitaa hapa karibuni na hata chaguzi nyingine za nyuma na
kuweka misimamo yetu ya watu wanaotufaa. Tukumbuke kwamba ofisi za
bunge, udiwani n.k siyo kituo cha ushauri nasaha kwamba mtu mwenye tabia
zisizokubalika akiingia pale atapewa ushauri na kuacha tabia zake
mbaya. Hivyo tunapochagua mtu tuchague yule ambaye tayari
ametengenezeka. Jamii yetu ya kitanzania ina watu wenye uelewa na uwezo
wa kuwahudumia wananchi kwa nini tusiwashawishi watu hao waingie kwenye
kinyang’anyiro na tuwahakikishie ushindi? Au ni kwa kuwa mara nyingi
watu hao wanakuwa hawana mpango wa kutukirimu?
Tuwe makini na watu wanaokuja na hoja za kwamba
wamegundua kuna mapungufu haya na yale katika uongozi wa mtu ambaye kwa
wakati huo yuko madarakani. Tuwashukuru waibua mabaya na kuyaweka
hadharani kwani wanasaidia kutuonesha wale wanaotufilisi na kutufanya
tuishi katika maisha duni. Kwa hilo tuwaambie asante na ikiwezekana
tuwazawadie kwa kazi hiyo. Lakini kamwe hilo lisiwe ndiyo kigezo namba
moja cha kuwapa nafasi za kutuongoza katika maeneo yetu. Sisi
tunachokihitaji ni mtu mwenye uwezo wa kutupunguzia au kutuondolea
maumivu yetu basi.
Ni ukweli kabisa kwamba hao wanaotafuna rasilmali
zetu wanachangia kwa kiasi kikubwa kutuongezea makali katika yale ambayo
kwa sasa tunaumia lakini bado nasema haiwezekani kumpa mtu nafasi kwa
sababu tu amefanikiwa kumshika mwizi lakini hana sifa nyingine yoyote ya
kutuongoza. Tuwaombe wale wanaokuja kujinadi kwamba pamoja na kutupa
taarifa ya wezi wa nchi hii watuambie namna wao wanavyoweza kutupunguzia
maumivu yetu. Ile kumkamata mwizi na kumwanika hadharani kunaonesha
uzalendo, pengine hata uadilifu kama huyo msemaji naye hana tabia hizo
lakini bado hakutoi kiongozi bora. Uadilifu pekee haufanyi mambo yaende;
tunahitaji mtu ambaye ana uwezo wa kuzilinda hizo rasilmali lakini
kikubwa awe na ubunifu wa kuzitumia kwa namna ambayo utaleta maendeleo
katika jamii zetu.
Tukilaghaiwa kuchagua watu ambao kila kunapokucha
kazi yao ni kusema tu nani kaiba, nani kaficha basi tujue kuna uwezekano
mkubwa kwa watu hao kuendelea kututajia watu waliotuibia bila kutupa
suluhu yoyote ya matatizo yetu kwa kipindi chote cha miaka mitano. Na
hapa naomba nieleweke vizuri kwamba sijaribu hata kidogo kuwaponda
wanaoibua wezi la hasha. Ninachotaka nieleweke ni kwamba anayetaka
uongozi asiegemee tu kwenye ujasiri wake wa kuwataja wezi hadharani
kwani hiyo ni sifa ya ziada; anahitajika kuwa na sifa zitakazochangia
katika kuondoa kama siyo kufuta kabisa kero zetu kwani ubora ndio tunda
tunalotaka kuliona.
Post a Comment