Ukawa watikisa: CUF yatoa vifaa, yapeperusha bendera ya Afro Shiraz Zanzibar

Z’bar/Dar. Chama cha Wananchi (CUF) jana  kilionyesha jinsi kilivyojiandaa kwa “mwaka wa uamuzi” wakati kilipogawa vifaa mbalimbali vya kusimamia kuwezesha wanachama wake kusimamia Uchaguzi Mkuu katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na maelfu ya watu kwenye Uwanja wa Mnazi Mmoja.
CUF, moja ya vyama viwili vikubwa visiwani Zanzibar, iligawa magari kwa kila wilaya na kamati  zilizoteuliwa kusimamia uchaguzi, pikipiki aina ya Vespa kwa majimbo yote 50 na katibu mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharrif Hamad alisema lengo la mgawo huo ni kuutangazia umma kuwa “huu ni mwaka wa uamuzi”.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa uzinduzi wa Kamati za Uchaguzi za chama hicho kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja, Maalim Seif alisema safari ya uchaguzi tayari imeanza na CUF imejipanga vizuri kuliko chaguzi zote zilizopita na imeamua kutumia miezi minane iliyobakia kukamilisha mkakati wa ushindi.
Alisema kuzinduliwa kwa kamati hizo za Uchaguzi Mkuu ni kuanza safari ya Zanzibar kupata mamlaka kamili na kuongeza “hakuna kuremba ni kazi, kazi, kwa sababu Wazanzibar wanaitegemea CUF kuwakomboa”.
Alisema wamejipanga, wamejizatiti kwa kila hali wala hakuna kinachowatisha na azma ya kutimiza wanachokitaka itatimia kwa umoja wao.
CUF imekuwa ikitoa upinzani mkubwa katika kila uchaguzi tangu kurejeshwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi, na CCM imekuwa ikipata ushindi wa tofauti ndogo ambao mara zote umekuwa ukilalamikiwa, hali iliyosababisha vyama hivyo kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya machafuko kutokea mwaka 2005.
“Sitaki visingizio, nimewapa vitendea kazi; magari, pikipiki, mashine za kutolea nyaraka mbalimbali, mashine za matangazo (PA)  sasa kafanyeni kazi huku mkiyakumbuka maazimio yetu ya mwaka huu ambayo ni kazi kwa kwenda mbele. Huu siyo mwaka 2005, wala 2010. Huu ni mwaka 2015, mwaka tofauti kwa chama chetu,” alisema Maalim Seif.
Maalim Seif, ambaye alihutubia kwa  zaidi ya saa moja na nusu, aliamsha shangwe na vigeregere kutoka kwa watu waliohudhuria mkutano huo wa uzinduzi wakati aliposema kuwa wanaungana na tamko la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kutoshiriki katika upigaji Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
Katibu Mkuu huyo alisema kuwa katika kuhakikisha huu ni mwaka wa uamuzi na siyo wa uchaguzi, wananchi wa Zanzibar wasishiriki kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa kwa sababu siyo yao badala yake wajipange kuhakikisha Chama hicho kinashika dola.
“Wamepiga ngoma wenyewe, wamecheza wenyewe, tuwaache waipigie kura wenyewe. Katiba hiyo ni ya Dodoma na itabaki huko,” alisema Maalim Seif.
Alisema wananchi wamechoka kutawaliwa na utawala usio na upeo, dira, uadilifu, ubunifu, na mwelekeo, chama kisichojiamini, kinachoshindwa kusimama kidete kutetea masilahi ya Wazanzibari.
Alifafanua kuwa CUF ipo tayari na imejipanga kwa ajili ya kutetea masilahi ya wananchi wote, kufanya uamuzi ndani ya Zanzibar badala ya kufanyia Dodoma.
- Zaidi Hapa Mwananchi

Post a Comment

أحدث أقدم