Kaniki: Najipanga kumrithi January Makamba Jimbo la Bumbuli

Wakati Mbunge wa Bumbuli, January Makamba akitangaza nia ya kugombea urais mwaka huu, kada wa CCM Abdul Kaniki ametangaza nia ya kugombea ubunge kwenye jimbo hilo kumrithi.
Hatua ya Kaniki inafungua ukurasa mpya wa upinzani ndani ya CCM katika jimbo hilo ambalo mwaka 2010, lilikuwa na wagombea wanane, akiwamo aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, William Shelukindo ambaye alishindwa katika kura za maoni.
Kaniki alikuwa miongoni mwa makada hao waliochuana vikali kumrithi Shelukindo, kabla ya Makamba kushinda nafasi hiyo bila kupingwa na upinzani.
“Bado kiu yangu ya kuleta maendeleo katika jimbo hilo maarufu kwa kilimo cha chai na matunda haijafa. Hivyo, nitarudi tena kwenye kinyang’anyiro cha ubunge mwaka huu kumrithi Makamba,” alisema.
Kaniki anataja agenda yake kuu kama atashinda ubunge kuwa ni kushirikisha wananchi katika kuleta maendeleo katika nyanja mbalimbali, ikiwamo kilimo, maji, umeme, barabara, elimu na afya.
Katika kilimo, kada huyo (38) anaonyesha kusikitishwa kwa sekta hiyo kudidimia, hasa baada ya Kiwanda cha Chai Mponde kufungwa na baadhi ya wakulima kukata tamaa.
“Nikipewa dhamana, kitu cha kwanza ni kuimarisha mtandao wa kukifanya kilimo chenye tija. Unapozalisha ni lazima uhakikishe kuna watumiaji,” alisema.
“Kiwanda kikifunguliwa kitaleta ari zaidi kwani mkulima akiuza chai yake atakuwa ana uwezo wa kununua unga, kulipia gharama za elimu, kufanya biashara zake na hatimaye kuboresha maisha yake kwa ujumla.”
Alisema wakulima wa chai katika Jimbo la Bumbuli walisusa kuzalisha zao hilo wakishinikiza serikali itatue mgogoro wao kwanza wa kunyanyaswa na kupatiwa ujira ndogo.
Kaniki, ambaye ni msomi mwenye Shahada ya Sayansi ya Uhandisi wa Mawasiliano kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alisema kuwa kuna kazi nzito ya kuwavutia wakulima waliokata tamaa warudi kuendelea na kilimo. “Hii ni kazi kubwa inayohusiana na saikolojia. Wakivutiwa kurudi tutawahamisisha walime pia mahindi na matunda kwa kuwa Bumbuli ina sehemu kubwa ya maji yanayotiririka na kustawisha mazao mbalimbali,” alisema na kuongeza kuwa Makamba kashindwa kufanya hilo kikamilifu.
Kwa mujibu wa Kaniki, uhamasishaji huo utaenda sambamba na kuhakikisha vijana wanaohitimu darasa la saba na kidato cha nne wanaacha kuendesha bodaboda na kuingia kwenye kilimo.
Anabainisha kuwa kama mwanasiasa kijana, mzawa wa Bumbuli anaongozwa na “dhamira, ari na ubunifu katika ushirikishaji wananchi” ambavyo vitasaidia pia katika kukusanya mapato mbambali ya kuendeleza miradi ya jimbo.

Post a Comment

أحدث أقدم