NEC yakamilisha uandikishaji Halmashauri ya Makambako.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec)
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imemaliza kuandikisha wapigakura kwenye daftari la kudumu kwa mfumo wa kielektroniki (BVR), katika Halmashauri ya Mji wa Makambako, mkoani Njombe katika kata tisa na kuendelea kwa wiki mbili katika kata za pembezoni za halmashauri hiyo. 
 
Akizungumza na NIPASHE, Mkurugenzi wa Halmashauri ya mji wa Makambako, Vumilia Nyamoga, alisema uandikishaji umemalizika na umefungwa katika kata tisa na kwamba uandikishaji utaendelea katika kata za Kitandililo ambako ulianza juzi. 
 
Alisema kata nyingine ambako uandikishaji ulianza jana ni kata ya Mahongole ambako utaendeshwa kwa wiki moja. Katika kata ya Utengule uandikishaji utaendeshwa wiki moja baada ya kumalizika kata hizo mbili. 
 
“Kwa mji wa Makambako ulieenda vizuri kwa siku hizi mbili za nyongeza na tunaweza kusema wamekamilika wananchi wote kwa kuwa kwa siku ya leo (jana), ambayo ni ya mwisho baada ya kuongezeka kwa siku mbili watu wamepungua kabisa,” alisema mkurugenzi huyo. 
 
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Makambako, Chesco Mfikwa, alisema uandikishaji kwa siku hizo mbili wananchi waliendelea kujitokeza na kuwa siku ya mwisho ya nyongeza wananchi walijitokeza wachache tofauti na siku ya kwanza ya nyongeza. 
 
Alisema hadi juzi, walikuwa wamewaandikisha wakazi 44,227 wa kata tisa ambazo uandikishaji ulianzia.
 
Mmoja wa waandikishaji katika kituo kimoja katika kata ya Mjimwema, alisema kwa siku mbili walizoongezewa kuna wananchi 115 kwa siku ya kwanza na siku ya pili kufikia saa saba walikuwa na watu 50 waliowaandikishwa na kuwa walikaa katika kituo hicho kwa muda zaidi ya saa tatu bila kuja mtu kuandikisha. 
 
“Kwa siku ya leo (jana) watu 50 tu wamefika tangu ashubuhi, lakini kwa siku ya jana watu 115 tuliwaandikisha na watu hawa isingekuwa kuongezwa muda watu hawa wasinge kuwa wameandikishwa,” alisema ofisa huyo ambaye hakutaka jina lake kutajwa.
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

أحدث أقدم