Yanga yanasa pabaya

YANGA inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara kesho Jumatano inaanza mwezi mgumu wa April ambapo ikicheza karata zake vizuri itajihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa mwakani, lakini ni mwezi wa kutengeneza heshima pia kwa Mwarabu.

Ni mwezi ambao Yanga kama ikiimaliza FC Platinum ya Zimbabwe ina uwezekano mkubwa wa kukutana na Etoile du Sahel ya Tunisia, ambayo ni moja ya timu ngumu za kiarabu zinazosumbua Waswahili lakini mwezi huo ndiyo ambao Yanga inaweza kujijengea au kujiharibia.

Yanga inaongoza ligi ikiwa na pointi 40 huku ikihitaji kushinda mechi nne tu kujihakikishia kushiriki tena michuano hiyo tofauti na Simba ambayo hata ikishinda mechi zote sita zilizobaki itafikisha pointi 50 wakati Yanga waliobakiza mechi saba watafikisha pointi 53 kwa kushinda mechi nne.

Mwezi ujao, Yanga itakuwa na mechi tatu kama hakutakuwa na mabadiliko yoyote kwenye ratiba ya ligi wakati Simba wao watacheza mechi nne ambapo mbili zitachezwa nyumbani na nyingine mbili ugenini kati ya Kagera Sugar itakayochezwa Uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga Jumamosi na ile ya Aprili 18 dhidi ya Mbeya City itakayochezwa Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Mechi za nyumbani ni dhidi ya Mgambo Shooting itakayochezwa wiki ijayo, April 12 na ile ya Ndanda United itakayochezwa April 25, zote zitapigwa Uwanja wa Taifa. Mechi zote ni ngumu kwa Simba kwani wanapaswa kucheza kila wiki.

Yanga wenyewe mwezi ujao mechi zote zitachezwa nyumbani Uwanja wa Taifa ambapo wakirejea kutoka Zimbabwe wataanza na Mbeya City, Coastal Union na Ruvu Shooting.

Kwa kufuata hesabu za msimamo wa ligi, Yanga bado wataendelea kutesa mwezi ujao kama watashinda mechi zote tatu na kukusanya pointi 49 na kama watapoteza mechi bado wataizidi Simba ambao hata wakishinda mechi zote nne watafikisha pointi 44 hata kama Yanga watapoteza moja Simba hawatafikia pointi za Yanga kwa mwezi huu.

Yanga wanatarajia kuondoka usiku wa kuamkia keshokutwa Alhamisi kwenda kucheza mechi ya marudiano dhidi ya Platinum ya Zimbabwe ambapo mechi ya awali Yanga ilishinda mabao 5-1 wakati Simba wao wataondoka kesho Jumatano kuelekea Shinyanga kuwafuata Kagera Sugar.

Kumbukumbu zinaonyesha kuwa ni mwezi mmoja na ushei Simba imetoka kupokea kichapo cha bao 1-0 mjini Shinyanga mbele ya Stand United katika uwanja utakaowakutanisha na Kagera Sugar yaani CCM Kambarage.

Post a Comment

Previous Post Next Post