APOTEZA FAHAMU KWA MIEZI MIWILI

JOSEPH Matitu anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 50  ambaye hajajulikana kuwa ni mkazi wa wapi, ameokotwa na wasamaria wema Machi 13, mwaka huu baada ya kudondoka ghafla na kupoteza fahamu.
Joseph Matitu anayedaiwa kupoteza fahamu kwa miezi miwili, akiendelea kupata matibabu.
Kwa mujibu wa mtoa habari wetu, Matitu aliokotwa Kibaha, mkoani Pwani baada ya watu kumuona akiwa amelala chini, wakahisi alikuwa amefariki dunia.
Hata hivyo, baada ya kumsogelea walimuona akipumua lakini akiwa hajitambui, wakachukua jukumu la kumkimbiza katika Hospitali ya Tumbi, Kibaha kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
AHAMISHIWA MUHIMBILI
“Mzee huyo alipofikishwa katika hospitali hiyo, madaktari walimlaza kwa siku mbili, hata hivyo baada ya kuona hali yake inazidi kudorora, uongozi uliamua kumhamishia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi akiwa hajitambui,” alisema mtoa habari kwa sharti la kutoandikwa jina gazetini.
Ilielezwa kuwa mzee huyo alianza matibabu katika hospitali hiyo Machi 16, mwaka huu lakini hadi leo hajapata ndugu zake wala anapoishi hapajulikani.
Baada ya kufikishwa katika hospitali hiyo, madaktari walianza matibabu, hata hivyo, hali yake hadi sasa bado ni mbaya japokuwa amepata fahamu na anaongea kwa tabu baada ya kupoteza fahamu kwa miezi miwili.
Mmoja wa wauguzi  katika wodi 1 ya Mwaisela ambaye  hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alisema mgonjwa huyo hadi sasa hawezi kuongea japokuwa ana nafauu ukilinganisha na jinsi alivyoletwa akitokea Tumbi, Kibaha.
Afisa Ustawi Jamii wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Grace Julius anayesimamia Wodi 1 ya Mwaisela alisema mgonjwa huyo anaendelea vizuri.
“Hadi  sasa Matitu hajapata ndugu hivyo yeyote aliyepotelewa na ndugu afike kumtambua,” alisema Grace.
Afisa Habari Mkuu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Aminiel Aligaesha alisema kuwa kazi ya hospitali hiyo ni kuhakikisha kila mtu anapata matibabu kadiri inavyowezekana awe ana ndugu au hana.
WITO KWA UMMA “Anayemfahamu  Joseph Matitu ajitokeze au awajulishe ndugu zake wa karibu kama anawafahamu au wafike Muhimbili Wodi 1 ya Mwaisela,” alisema.
Kwa yeyote aliyeguswa na habari hii awasiliane na Ofisi ya Ustawi wa Jamii Muhimbili kwa namba O765 409 575.

Post a Comment

Previous Post Next Post