CCM yatajwa biashara ya dawa 'feki' za Wakorea.

Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Dar es Salaam kinakabiliwa na kashfa ya kushirikiana na kliniki binafsi za raia wa Korea Kaskazini, zinazodaiwa kuuza dawa zinazoathiri afya na maisha ya watu.
 
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa miezi kadhaa, umepata taarifa za vyanzo tofauti zinazoelezea upungufu wa kitabibu kwa dawa zinazotolewa na kliniki hizo, hususani zilizopo Temeke, Magomeni na Kariakoo jijini humo, lakini serikali haijachukua hatua zozote za udhibiti.
 
Taarifa za hivi karibuni zinaeleza kuwa baada ya kufichuliwa kwa upungufu huo, wamiliki wa kliniki hizo wanatumia muda mwingi kutoa taarifa kwa wagonjwa wanaofika, wakikanusha kuhusu upungufu na madhara yanayotajwa kuwapo kwenye dawa zao. Pia wanakitumia CCM kama kinga ama ushawishi kwa umma kwamba utendaji wao unakidhi matakwa ya sheria na kanuni za tiba.
 
Gazeti hili limepata nakala ya barua moja iliyoandikwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwenda CCM mkoa wa Dar es Salaam, kujibu ombi la kutaka kliniki hizo kuruhusiwa kutoa pia huduma za tiba za kisasa.
 
Barua hiyo (kumbukumbu namba na ofisa aliyeisaini tunavihifadhi kwa vile hajapatikana kuielezea), ilionyesha kujibu barua ya CCM mkoa wa Dar es Salaam ikiwa ni mmiliki wa kliniki hiyo.
 
Pamoja na mambo mengine, ilieleza ombi la CCM kutaka kampuni ya Maibong-Sukidar inayomilikiwa na chama hicho kutoa tiba kutumia dawa za kisasa na asilia kutoka Korea.
 
Barua hiyo ya wizara inaeleza msimamo wake kwamba kliniki hiyo ilipewa kibali kutoa tiba asilia kutoka Korea na kwamba kama kulikuwa na hitaji la kutoa tiba za kisasa, ilipaswa kuwasilisha vielelzo vinavyothibitisha kuwa madaktari na wafamasia wake wana uelewa kuhusu tiba za kisasa.
 
Hata hivyo, bado haijathibikika kama agizo hilo la wizara lililotolewa mwaka 2008 lilifanyiwa kazi na CCM au kliniki hiyo.
 
Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Abilah Mihewa, amethibitisha chama hicho kuingia ubia na Wakorea Kaskazini katika biashara ya kliniki hizo, ingawa miongoni mwa makubaliano yaliyofikiwa na uongozi uliopita yanafanyiwa kazi.
 
Mihewa alisema kwa upande wa Temeke, CCM ilikubaliana na Wakorea hao kuwekeza kwenye ardhi yake na kwamba CCM haihusiki na shughuli za uendeshaji na utoaji huduma za afya.
 
Hata hivyo, Mihewa alisema kliniki iliyopo Magomeni Mikumi, uongozi wake bado haujapata uthibitisho wa namna CCM inavyoshiriki ikiwa ni kwa umiliki wa ardhi pekee au pamoja na majengo.
 
Alisema hali hiyo inatokana na hatua za makubaliano ya biashara hiyo kufanywa na uongozi uliopita ambapo mpaka sasa ofisi yake inaendelea kulishughulikia suala hilo ili kupata ufumbuzi wa kudumu.
 
HOFU YA KUPOTEZA KURA
Sakata hilo linadaiwa kuwa huenda likaibua madhara kama upofu, kupoteza fahamu, mwili kulegea na kuwa kiziwi  kwa watu baada ya muda mrefu, zinazidi kukiweka chama hicho katika hatari ya kutoungwa mkono katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu. Hali hiyo inatokana na jinsi CCM, serikali na mamlaka husika zilivyoshindwa  kushughulikia kero mbalimbali za kijamii na kusababisha kupoteza viti vingi wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa.
 
Waziri wa Afya na Ustawi na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid na Meneja Ukaguzi na Udhibiti wa Dawa na Vipodozi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kanda ya Mashariki, Emmanuel Alphonce, hawakupatikana kuelezea sakata hilo.
 
Lakini Mkurugenzi Mkuu wa TFDA, Mkurugenzi Mkuu wa TFDA, Hiiti Sillo aliwahi kuliambia gazeti dada la The Guardian hivi karibuni kuwa ukaguzi dhidi ya tuhuma hizo ungefanywa na mamlaka hiyo, lakini hakuna taarifa kuhusu utekelezaji wake.

Post a Comment

Previous Post Next Post