Chadema: Hakuna kulala, hakuna kula

Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jana kilizindua mkakati wake wa ushindi “Hakuna kulala, hakuna kula mpaka kieleweke” katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba kwa kufungua mafunzo yatakayoendeshwa nchi nzima kwa viongozi wa vyama na Serikali za Mitaa.
Katika mkakati huo, chama hicho kimeigawa nchi katika kanda 10 za utekelezaji huku kikijipanga kuimarisha nguvu zaidi katika Jiji la Dar es Salaam lenye idadi kubwa ya wapigakura.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema wakati wa uzinduzi wa mkakati huo kitaifa jijini hapa kuwa watafundisha viongozi wote wa chama hicho na watangaza nia, mbinu za uongozi bora na namna ya kushinda.
Mbowe alisema mpango huo wa mafunzo ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya chama kwa kuwa hawawezi kushika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa bila kuwa na viongozi bora na weledi.
Alisema Chadema kitakwenda katika kanda zote, majimbo ya kichama 242, kata 4,852, matawi 22, 749, misingi 64,803 na kuwafikia viongozi 224,287 na timu zote za mafunzo zimeshatawanyika nchi nzima.
“Tunawafundisha viongozi wetu walio tayari ndani ya chama au Serikali za Mitaa namna ya kutekeleza wajibu wao. Lakini tunawaimarisha wanaokusudia kugombea nafasi mbalimbali kuwa wagombea wazuri zaidi, kuandaa ajenda za chama na namna ya kukamata madaraka kwa kuwa safari ya kushika Dola 2015 haina kizuizi,” alisema Mbowe huku akishangiliwa.
Kuahirisha uchaguzi
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na mamia ya viongozi na watia nia wa Kanda ya Pwani ya chama hicho, Mbowe aliitaka Serikali kutojaribu kabisa kuahirisha Uchaguzi Mkuu kwa sababu ya kusuasua kwa uandikishaji wa daftari la kudumu la wapigakura kwa kutumia teknolojia ya Biometric Voters Registration (BVR) akitishia kuwa ‘moto utawaka’.
Alisema Ukawa hawakusema chochote wakati wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilipoahirisha Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa kwa kuwa ilikuwa batili na ilianzishwa kwa masilahi ya Serikali na aliahirishwa na wao wenyewe.
Aliitaka Serikali kuharakisha uandikishaji wa daftari la kudumu la wapigakura kwa kuwa imesalia miezi mitatu na nusu kabla ya kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu hapo Agosti.
Alisema tarehe ya kupiga kura ambayo ni Jumapili ya Oktoba ilifahamika tangu awali kwa kuwa ni ya kikatiba lakini mpaka sasa uandikishaji unasuasua katika Mkoa wa Njombe wenye wapiga kura 340,000 ambao alisema hawafiki hata nusu ya waliopo Jimbo la Ubungo.
“Wanasubiri kama walivyofanya kwenye kuahirisha Kura ya Maoni na ili waseme ‘ndugu Watanzania kwa kuwa tumechelewa kuandikisha wapigakura tunaomba Bunge lako tukufu liongezee muda kwa Serikali ya awamu ya nne’... mtakubali?” aliwahoji wafuasi hao na kujibiwa “Hapanaaaa”

Post a Comment

Previous Post Next Post