Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima,amesema haogopi
mtu yeyote wala kufa bali ataendelea kuinyoosha nchi anapoona haiendi
sawa.
Alitoa kauli hiyo Dar es Salaam jana,wakati wa mahubiri yaliyofanyika katika Viwanja vya Tanganyika Packers Kawe.
Alisema uhusiano wake na watu mbalimbali wakiwamo wanasiasa utaendelea kubaki palepele.
Kwa mujibu Askofu Gwajima, baadhi ya watu wamekuwa wakimhusisha kuwa na
urafiki na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowasa jambo ambalo alikiri ni
la ukweli kwa sababu walifahamiana tangu mwaka 1996.
“Niliwahi kumuita Waziri Mkuu Mizengo Pinda mara nne hapa ili aje
azindue moja ya kazi zangu,hakuja badala yake nilimuita Lowassa na
aliitikia wito wangu na kuja kuifanya kazi hiyo hivyo siwezi kumuacha.
“Wapo viongozi wengi ambao wanakuja kusali katika kanisa langu, kwa
mfano Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM,Nape Nnauye, kwa nini wasimseme
yeye badala yake wanamsema Lowasa tu?.
“Nashangaa mnatoka mlipotoka mnaongea kwa kubana pua, ukimuogopa mtu
nchi itakuwa haiendi vizuri na mimi sitaogopa kukemea mambo ambayo
hayafai katika jamii, mfano suala la Escrow.
“Nitaendelea kuinyoosha nchi ninapoona haiendi sawa.
“Siwezi kwenda mbali na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk.Willbrod Slaa hata
kama atakuwa Rais… na yeye pia ni rafiki yangu,” alisema Askofu Gwajima.
Katika ibada hiyo aliliombea Taifa amani, uchaguzi mkuu unaotarajiwa
kufanyika Oktoba mwaka huu na kikao kijacho cha Bunge la Bajeti
linalotarajia kuanzia baadaye mwezi ujao.
Wiki iliyopita, Askofu Gwajima alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu kwa mashitaka mawili ambayo ni kumtolea lugha ya matusi
ambayo imemfedhehesha Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es
Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, na kuweka vibaya silaha
anayomiliki.

إرسال تعليق