Hatima ya makada sita wa CCM leo

Dodoma. Kamati Kuu ya CCM, ambayo ndiyo inaanzisha mambo yote muhimu ya chama hicho, leo inakutana kuandaa ajenda za mkutano wa Halmashauri Kuu, huku suala linalosubiriwa kwa hamu likiwa ni hatima ya makada sita wanaotajwa kuwania urais ambao wanatumikia adhabu ya kuzuiwa kujihusisha na uchaguzi.
Kwa mara ya kwanza, CCM inakabiliwa na kazi ngumu ya kuamua hatima ya makada iliowafungiwa katika kipindi muhimu cha kuteua mgombea mpya wa urais kutokana na mwenyekiti wa sasa wa chama hicho, Jakaya Kikwete kutoweza kugombea nafasi hiyo kwa kipindi cha tatu kutokana na matakwa ya kikatiba.
Mmoja wa watu walio karibu na uongozi wa chama hicho aliiambia Mwananchi jana kuwa CCM imejikita zaidi katika kutafuta mwanachama atakayekipa ushindi kwenye Uchaguzi Mkuu, lakini suala la makada waliofungiwa ambao baadhi yao wanapewa nafasi kubwa ya kupitishwa, halitachukua muda mrefu kulijadili.
Kikao hicho kitafanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri Kuu uliopo jengo la makao makuu ya CCM mjini hapa, maarufu kama White House mjini Dodoma.
Ukumbi huo una historia ya muda mrefu ndani ya CCM ya kutolewa kwa uamuzi mgumu katika matukio kadhaa ya kisiasa, ukiwamo ule ulioweka historia ya Aboud Jumbe kuingia akiwa Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, lakini akatoka bila cheo chochote mwaka 1984.
Pia kwenye ukumbi huo kulifanyika uamuzi wa mambo mengine makubwa, hasa nyakati za kuchuja wagombea urais au uongozi wa chama, mambo ambayo pia yanaweza kutokea katika vikao vinavyoanza leo au vya baadaye.
Alipoulizwa kuhusu kikao hicho jana, katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema Rais Kikwete ataongoza kikao cha leo kilichopangwa kuanzia saa 4:00 asubuhi na kwamba maandalizi yamekamilika, huku baadhi ya wajumbe wakiwa wameshawasili.
Alipoulizwa kuhusu nini wategemee wanachama na wananchi, Nape alijibu kwa kifupi kuwa watarajie kuwa “CCM watatoka wakiwa kitu kimoja” kuliko inavyotarajiwa na wengi.
Hata hivyo, mbali na hofu kuhusu hatua za kinidhamu kwa wajumbe walioadhibiwa kwa kuanza kampeni mapema na kukiuka maadili, taarifa nyingine kutoka kwa baadhi ya wajumbe wa vikao hivyo zilidai kuwa mkutano huo utajikita zaidi kuangalia utaratibu mzima wa kuchukua fomu za wagombea wote wa urais, ubunge na udiwani.
“Vikao hivi vinaangalia utaratibu tu wa jinsi ya kuchukua fomu na wala havitagusia suala la mchujo wa wagombea urais wala ubunge,” alisema mtoa taarifa huyo.
Kamati Kuu imetanguliwa na vikao vya mfululizo vya Sekretarieti na Kamati ndogo ya Kanuni.
Kamati ya Kanuni na Maadili ilitarajiwa kukutana jana usiku au leo asubuhi kabla ya Kamati Kuu.

Post a Comment

Previous Post Next Post