NANI NI NANI URAIS: Fahmi Dovutwa: Mwenyekiti wa chama cha UPDP

Fahmi Nasoro Dovutwa ni Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP). Alizaliwa Februari 27, 1957 mjini Kisarawe mkoani Pwani (Amefikisha miaka 58 Februari mwaka huu).
Dovutwa alianza elimu yake ya msingi mwaka 1967 katika shule ya msingi Zanaki hadi alipohitimu mwaka 1974 alipoendelea na masomo ya sekondari katika shule ya sekondari Azania ambako alihitimu mwaka 1977.
Rekodi za elimu za Dovutwa zimekuwa “kizungumkuti” kupatikana. Hata taarifa zake binafsi alizotoa kwa ajili ya rekodi za Bunge Maalum la Katiba zinasisitiza kuwa ameishia kidato cha nne.
Juhudi za kumpata yeye mwenyewe ili akamilishe rekodi zake hazikufua dafu na ni yeye peke yake tangu nianze kufanya uchambuzi wa watu wanaotajwa kuwania urais, ambaye hakutoa ushirikiano kabisa ili kunifanya nipate rekodi zake sahihi. Hata hivyo hilo haliwezi kunizuia kumchambua.
Watu wa karibu yake wamenijulisha kuwa kwa muda mrefu amekuwa akijishughulisha na kazi za ujasiriamali katika soko la Magereza jijini Dar es Salaam hadi baadaye alipochaguliwa kuongoza chama cha UPDP ambacho yeye ni mwenyekiti hadi sasa.
Mwaka 2014, alikuwa ni miongoni mwa Watanzania waliopata fursa ya kuteuliwa na Rais wa Tanzania kupitia kundi la vyama vya siasa, na kuwa mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba lililofanya kazi yake mjini Dodoma na kukamilisha Katiba Inayopendekezwa ambayo hata hivyo imeligawa taifa katika vipande viwili. Dovutwa ameoa na ana watoto.
Mbio za ubunge
Katika historia ya kisiasa ya Dovutwa, hakutoa pia rekodi zinazoonyesha kama aliwahi kugombea ubunge katika jimbo lolote na hata nilipozitafuta sikufanikiwa kuzipata.
Mbio za urais
Kiongozi huyu alijitosa katika mbio za urais mwaka 2010 akitumia tiketi ya chama chake cha UPDP. Katika uchaguzi ule ambao Jakaya Mrisho Kikwete aliongoza kwa ushindi wa asilimia 62.83, akifuatiwa na Willibroad Slaa aliyekuwa na ushindi wa asilimia 27.5, na Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF akiwa na asilimia 8.28, Dovutwa aliibuka katika nafasi ya mwisho akiwa na asilimia 0.16 ya kura zote kwa kupitwa na Peter Mziray wa APPT (asilimia 1.15), Hashim Rungwe wa NCCR (asilimia 0.31), na Mutamwega Bhatt wa TLP aliyekuwa na asilimia 0.21 ya kura zote.
Katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, Dovutwa hajatangaza popote kuwa atagombea tena nafasi ya urais lakini duru za kisiasa ndani ya chama hicho ikiwamo kutoka kwa baadhi ya viongozi waandamizi, zimenieleza kuwa anapewa nafasi kubwa ya kugombea tena.

Post a Comment

Previous Post Next Post