Sitti Mtemvu, Miss Tanzania wa kwanza katika 
historia ya shindano hilo kutema taji la urembo, anazindua kwa mpigo 
'shirika' lisilo la kiserikali la misaada ya kijamii, kitabu na kipindi 
cha TV jijini Dar es Salaam leo.
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Lazima tukubali, Nipashe, kwamba kitendo cha Sitti ambaye 
alilazimika kutema taji hilo mwaka jana baada ya kupata kashfa ya 
kupunguza umri wake ili aweze kushiriki shindano la Miss Tanzania, cha 
kuanzisha taasisi ya misaada kwa jamii, ni cha kuungwa mkono kwa 
asilimia 100 kutokana na uwepo wa watu wengi wenye mahitaji nchini.
Lakini, tunasikitika Nipashe, pamoja na nia njema ya mrembo huyo 
katika kuelekeza nguvu, uwezo na nafasi yake kwenye jamii katika kutoa 
chozi kwa ajili ya watu wenye mahitaji, hafla hii inakuja wakati ambao 
jina la mfadhili huyo linazidi kuchukiwa ndani ya jamii kadri siku 
zinavyokwenda mbele.
Ikumbukwe kuwa tuhuma za Sitti za kughushi umri ili ashiriki katika
 shindano la Miss Tanzania la mwaka jana zimeacha majanga ambayo mengi 
hayawezi kurekebishika tena.
Tuhuma zimeacha majanga nyuma ambayo mengi hayawezi kurekebishika 
tena kwa sababu, kwanza, shindano lenyewe la Miss Tanzania 
limesimamishwa kwa miaka miwili pamoja na makosa mengine, kuwapo kwa 
rekodi za vyeti viwili vya kuzaliwa vya Sitti vyenye kumuonyesha 
alizaliwa miaka miwili tofauti.
Kusimamishwa kwa Miss Tanzania kunaweza kuonekana kama baa 
lililowakumba Hashim Lundenga na Prashant Patel tu kutokana na fainali 
za shindano hilo kuwa moja ya matukio makubwa ya burudani nchini la kila
 mwaka lenye udhamini mnono.
Lakini ikumbukwe shindano la Miss Tanzania si tu ni chanzo cha 
ajira, hata kama ya muda, kwa washiriki, waandaaji na wasanii bali pia 
ni fursa ya biashara kwa wamiliki wa kumbi mbalimbali kuanzia ngazi za 
vitongoji mpaka taifa.
Aidha, ni wazi, kama Mamlaka ya Kodi (TRA) ni makini vya kutosha, 
kuna kiasi cha pato la taifa ambacho kitakuwa kimekosekana katika misimu
 mwili hii na yote, inasikitisha, ni kutokana na tuhuma za Sitti za 
udanganyifu wa umri.
Kibaya zaidi, madhara ya tuhuma za udanganyifu wa umri za Sitti 
hayaishii katika ngazi hizo za jamii na taifa kwa ujumla tu bali hata 
familia.
Tunasema madhara ya tuhuma za udanganyifu wa umri za Sitti yanagusa
 pia ngazi ya familia baada ya Ofisi ya Msajili wa Vifo na Vizazi (Rita)
 hivi karibuni kufafanua kuwa wafanyazi kadhaa wa wakala huyo ama 
walifukuzwa kazi, kusimamishwa au kupewa barua za karipio kali kutokana 
na tukio hilo.
Watoto na wategemezi wa mfanyakazi yeyote wa Rita aliyefukuzwa kazi
 kutokana na tuhuma za kusaidia kupatikana kwa cheti cha kughushi cha 
Sitti, basi, haitashangaza kama watakuwa wateja wa shirika na chozi vya 
mrembo huyo.
Tumpongeze tena Sitti kwa kuanzisha kitengo ambacho kinaweza kuja 
kuwa kimbilio la waathirika wa matendo yake ya awali endapo itathibitika
 mahakamani.
Lakini baada ya Rita kutimiza wajibu wake bila hofu wala upendeleo,
 tuchukue fursa hii, Nipashe, kutaka Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar
 es Salaam nalo litimize wajibu wake katika kuhakikisha mrembo huyo 
anafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zilizopo.
Kuacha Miss Tanzania, warembo, mawakala, wasanii, wamiliki kumbi za
 starehe, TRA na wafanyakazi na familia za wafanyakazi wa Rita wakiwa 
wahanga wa kitendo ya Sitti huku binti mwenyewe akipeta ndani ya jamii, 
ni dalili za kuwapo kwa matabaka ya watu nchini na haikubaliki.
Hatukutaja, makusudi, ukumbi ambapo uzinduzi wa Chozi la Sitti 
utafanyika lakini tuna hakika, Nipashe, polisi ina intelejensia ya 
kutosha kuufahamu kirahisi.
Sitti Mtemvu akamatwe.
     CHANZO:
     NIPASHE
    

Post a Comment