Sitti Mtemvu akamatwe.

Katuni.
Sitti Mtemvu, Miss Tanzania wa kwanza katika historia ya shindano hilo kutema taji la urembo, anazindua kwa mpigo 'shirika' lisilo la kiserikali la misaada ya kijamii, kitabu na kipindi cha TV jijini Dar es Salaam leo.
 
Lazima tukubali, Nipashe, kwamba kitendo cha Sitti ambaye alilazimika kutema taji hilo mwaka jana baada ya kupata kashfa ya kupunguza umri wake ili aweze kushiriki shindano la Miss Tanzania, cha kuanzisha taasisi ya misaada kwa jamii, ni cha kuungwa mkono kwa asilimia 100 kutokana na uwepo wa watu wengi wenye mahitaji nchini.
 
Lakini, tunasikitika Nipashe, pamoja na nia njema ya mrembo huyo katika kuelekeza nguvu, uwezo na nafasi yake kwenye jamii katika kutoa chozi kwa ajili ya watu wenye mahitaji, hafla hii inakuja wakati ambao jina la mfadhili huyo linazidi kuchukiwa ndani ya jamii kadri siku zinavyokwenda mbele.
 
Ikumbukwe kuwa tuhuma za Sitti za kughushi umri ili ashiriki katika shindano la Miss Tanzania la mwaka jana zimeacha majanga ambayo mengi hayawezi kurekebishika tena.
 
Tuhuma zimeacha majanga nyuma ambayo mengi hayawezi kurekebishika tena kwa sababu, kwanza, shindano lenyewe la Miss Tanzania limesimamishwa kwa miaka miwili pamoja na makosa mengine, kuwapo kwa rekodi za vyeti viwili vya kuzaliwa vya Sitti vyenye kumuonyesha alizaliwa miaka miwili tofauti.
 
Kusimamishwa kwa Miss Tanzania kunaweza kuonekana kama baa lililowakumba Hashim Lundenga na Prashant Patel tu kutokana na fainali za shindano hilo kuwa moja ya matukio makubwa ya burudani nchini la kila mwaka lenye udhamini mnono.
 
Lakini ikumbukwe shindano la Miss Tanzania si tu ni chanzo cha ajira, hata kama ya muda, kwa washiriki, waandaaji na wasanii bali pia ni fursa ya biashara kwa wamiliki wa kumbi mbalimbali kuanzia ngazi za vitongoji mpaka taifa.
 
Aidha, ni wazi, kama Mamlaka ya Kodi (TRA) ni makini vya kutosha, kuna kiasi cha pato la taifa ambacho kitakuwa kimekosekana katika misimu mwili hii na yote, inasikitisha, ni kutokana na tuhuma za Sitti za udanganyifu wa umri.
 
Kibaya zaidi, madhara ya tuhuma za udanganyifu wa umri za Sitti hayaishii katika ngazi hizo za jamii na taifa kwa ujumla tu bali hata familia.
 
Tunasema madhara ya tuhuma za udanganyifu wa umri za Sitti yanagusa pia ngazi ya familia baada ya Ofisi ya Msajili wa Vifo na Vizazi (Rita) hivi karibuni kufafanua kuwa wafanyazi kadhaa wa wakala huyo ama walifukuzwa kazi, kusimamishwa au kupewa barua za karipio kali kutokana na tukio hilo.
 
Watoto na wategemezi wa mfanyakazi yeyote wa Rita aliyefukuzwa kazi kutokana na tuhuma za kusaidia kupatikana kwa cheti cha kughushi cha Sitti, basi, haitashangaza kama watakuwa wateja wa shirika na chozi vya mrembo huyo.
 
Tumpongeze tena Sitti kwa kuanzisha kitengo ambacho kinaweza kuja kuwa kimbilio la waathirika wa matendo yake ya awali endapo itathibitika mahakamani.
 
Lakini baada ya Rita kutimiza wajibu wake bila hofu wala upendeleo, tuchukue fursa hii, Nipashe, kutaka Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nalo litimize wajibu wake katika kuhakikisha mrembo huyo anafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zilizopo.
 
Kuacha Miss Tanzania, warembo, mawakala, wasanii, wamiliki kumbi za starehe, TRA na wafanyakazi na familia za wafanyakazi wa Rita wakiwa wahanga wa kitendo ya Sitti huku binti mwenyewe akipeta ndani ya jamii, ni dalili za kuwapo kwa matabaka ya watu nchini na haikubaliki.
 
Hatukutaja, makusudi, ukumbi ambapo uzinduzi wa Chozi la Sitti utafanyika lakini tuna hakika, Nipashe, polisi ina intelejensia ya kutosha kuufahamu kirahisi.
 
Sitti Mtemvu akamatwe.
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

Previous Post Next Post